Mjomba akaiharibu siku

Mjomba akaiharibu siku

Ilikuwa ni mwaka 1987, wakati huo nilikuwa naishi na kaka yangu mkubwa maeneo ya Kinondoni Msufini. Basi siku moja asubuhi tukapata mgeni na hakuwa mwingine bali ni mjomba wetu ambaye alikuwa ni dereva wa malori makubwa huko Arusha. Sasa ilitokea kapata safari ya kuleta mzigo huku Dar na ndipo alipokuja kututembelea.Huyu Mjomba alikuwa na mdogo wake aliyekuwa akiishi Ilala na shughuli zake zilikuwa ni Kushona nguo pale pale Ilala. Lakini kwa bahati mbaya hakujua alipokuwa akiishi mdogo wake, hivyo kaka akanitaka nimpeleke mjomba kwa mdogo wake, kisha nirudi naye kwa sababu atalala hapo nyumbani.Tulipofika Ilala kwa mjomba mdogo, tukamkuta akikoboa Mahindi ya makande kwa kutumia kinu, na mkewe alikuwa amekaa na mashoga zake hapo hapo uwani wakisukana.

Nakumbuka ilikuwa ni siku ya Jumapili.Mjomba alifurahi sana kumuona kaka yake na alitukaribisha ndani na kutuagizia soda, na kisha akatoka zake nje kuendelea kukoboa mahindi. Mkewe aliingia ndani na mashoga zake na kututambulisha kwao kisha akatoka kuwasindikiza.Baadae alirudi na kundelea na shughuli za ndani huku mumewe akindelea kukoboa mahindi huko nje. Alipomaliza alimkabidhi mkewe yale mahindi ali ayabandike jikoni halafu akamuomba kaka yake tutoke kidogo kunyoosha miguu.Tulienda kwenye baa moja iliyokuwa mtaa wa pili, kwa ajili ya kupata moja moto moja baridi, kwa kuwa sinywi pombe niliagiza soda. Mjomba na mdogo wake waliagiza bia na kuanza kunywa huku wakipiga soga na kupeana habari za nyumbani.

Kumbe mjomba mkubwa alikuwa na dukuduku lake na pombe zilipomuingia ndipo akaanza kumpasha mdogo wake.‘Bwana mdogo unajua unanitia aibu, tena umenidhalilisha sana, yaani huyu Mzaramo wako amekutawala mpaka basi, hivi kweli wewe ni wa kukoboa mahindi na mkeo amekaa na mashoga zake wakisukana na kuchapa umbeya?’ Mjomba alianza kumfokea mdogo wake.Mjomba mdogo alitaka kumjibu lakini akamkata kalma na kumuonya asidhubutu kuongea mpaka amalize kuongea yeye…..

Basi mjomba akaendelea kumpasha mdogo wake kuwa anadhalilisha ukoo wao na kamwe hatakuja kwake na asije akafunga ndoa na huyo mwanamke kwa sababu hana maadili na hana heshima hata kidogo.Wakati wote mjomba mdogo alikuwa kajiinamia akimsikiliza kaka yake huku akiendelea kunywa bia moja baada ya nyingine.Nilijaribu kumnyamzisha mjomba, lakini wapi aliendelea kumfokea mdogo wake mpaka akatosheka, ndipo tukarudi nyumbani ili tupate chakula cha mchana kisha tuondoke kurudi Kinondoni.

Tulipofika tu Mjomba mdogo akamrukia mkewe na kuanza kumpiga huku akisema, “Mimi siku zote naishi na wewe kumbe umenitawala mpaka kaka yangu leo amenitolea uvivu na kunisema waziwazi, haiwezekani unitawale kiasi hicho…………….. na leo utanitambua” Wakati purukushani hizo zinaanza, wote tulishikwa na butwaa kwanza tusijue la kufanya, mara ghafla akaja jirani moja nakuingilia kati, na mjomba mkubwa naye akaanza kuamulia ule ugomvi, lakini mdogo wake aliendelea kubwabwaja yale maneno aliyoelezwa na mjomba mkubwa kule Baa……..

Binti wa Kizaramo naye hakukubali alikuwa akijibu mapigo na kuporomosha matusi akimtukana mjomba mkubwa waziwazi kuwa ni mbeya na mzandiki mkubwa aliyekwenda pale kuvunja uhusiano wao…….. alimwambia kama anadhani kuwa anafaidi basi atamvalisha khanga ili aolewe yeye…………….Majibizano yalikuwa ni makali na yenye kila aina ya kashfa na matusi ya nguoni yakimuhusisha mjomba mkubwa………………..ilibidi majirani wamuulize mjomba kulikoni anataka kuvunja uhusiano wa mdogo wake na mpenzi wake?

Mjomba hakuwa na la kusema alibaki kimya akiwa ametahayari. Alinishika mkono na kuniambia tuondoke kwani mambo yameharibika. Majirani walibaki kutuangalia wakati tunaondoka huku wakifyonya…………………. Ilikuwa ni fedheha kwetu

 






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Mzee Mtambuzi

A freelance Journalist and also teaching self-empowerment, positive thinking as a means of creating the life you desire including spirituality. He is writing in Mwananchi Scoop every Wednesday Visa na Mikasa.


Latest Post