Mavazi na muonekano bora zaidi kwa mama mjamzito

Mavazi na muonekano bora zaidi kwa mama mjamzito

Leo katika Fashion tutaelekeza jinsi gani mama mjamzito atakaweza kuwa na muonekano mzuri katika mavazi na aina ya mavazi anayotakiwa kuvaa katika kipindi hicho.

Baadhi ya wanawake wanapokuwa wajawazito hujiweka kando katika masuala ya mitindo na hata urembo hali inayopelekea kupunguza mionekano yao waliyokuwa nayo awali kabla ya kupata ujauzito.

Lakini wataalamu wa masuala ya mitindo na urembo wanaeleza kuwa ujauzito si kigezo cha kuacha kupendeza na kuvutia kama ilivyokuwa awali.

Akizungumza na Mwananchi Scoop mshonaji na mwanamitindo wa nguo za kike na kiume jijini Dar es Salaam, Jackline Maneno anasema kuwa na ujauzito siyo sababu ya  kuvaa nguo zisizovutia au kuacha kujiweka katika muonekano mzuri na unaopendeza anasema.

“Unakuta mtu kabla ya kuwa mjamzito alikuwa akivaa nguo nzuri, anajipenda hivyo anajitahidi kutunza ngozi yake anapopata ujauzito tu anaacha, hii haikuwa sawa kabisa,”alisema Jackkine.

Mwanadada huyo aliendelea kueleza kuwa ipo mishono na mitindo mbalimbali mingi, ipo katika mitandao na tovuti mbalimbali za mitindo, maalum kwa ajili ya wajawazito ambayo anaweza kushona na bado akapendeza na kwenda na ‘fashion’.

Alisema jambo la msingi kwa mjazito ni kujua na kukubali kuwa mwili wake utapitia mabadiliko mfano katika miezi ya mwanzo ya ujauzito alikuwa na mwili mwembamba anaweza kubadilika na kuongezeka kidogo mwili wake au kinyume cha hapo.

“Lakini pia ni muhimu kadri miezi inavyozidi kuyoyoma ndipo tumbo linavyozidi kuongezeka kutokana na mtoto anavyokuwa na pia anaweza kupitia mabadiliko mbalimbali kama kuvimba miguu,”alisema mwadada huyo.

Hivyo ni muhimu katika uvaaji wake kuzingatia size za nguo na viatu anavyovaa ili kumuweka huru kutokana na hali yake yaani hapa asikalili awali awe ni mtu wa kubadilisha mavazi kutokana na hali ya mwili wake utakavyo ongezeka.

Pia aligusia wajawazito wanaopendelea kuvaa nguo za kubana na kusema kuwa mavazi hayo si sahihi kwa mama mjamzito kwani anaweza kumfanya asiwe huru na hata kuchoka kwa haraka lakini pia si salama kwa afya yake na mtoto aliyeko tumboni kuna uwezekano  mkubwa mtoto akawa na shida kabla au baada ya kujifungua kama akibanwa sana anaeleza.

"Mjamzito anatakiwa kuvaa nguo inayomstiri mwili wake vizuri, pamoja na kuwa nguo za kubana sana mwili ni hatari kwake lakini pia haziendani hata na utamaduni wetu wa kiafrika,"

Kauli hiyo pia imeungwa mkono na daktari wa binadamu, Rachel Mwinuka ambaye anatueleza kuwa mama mjamzito anashauriwa kuvaa nguo zisizobana sana ili kuruhsu kupata mzunguko wa damu na hewa kwa urahsi kwa mtoto.

Lakini pia aligusia suala la wajawazito kuvaa viatu virefu kwa muda mrefu na kueleza kuwa uvaaji wa viatu hivyo vinaweza kumsababishia mama maumivu ya miguu na hata kuhatarisha usalama wa mama na mtoto aliyeko tumboni anasema daktari huyo.

"Anaweza hata akajikwaa na kudondoka na kuweza kusababisha maumivu ya tumbo na hata kumueka katika hatari mtoto aliyoko tumboni,"

Hivyo alishauri wanawake wajawazito wajitahidi kuepuka uvaaji wa viatu hivyo na wapendelee kuvaa viatu simple au flat shoes.

Hatukuishia hapo moja kwa moja tukapiga mbizi mpaka kwa mtaalamu wa masuala ya urembo , Isha Mtawa, anaeleza kuwa katika kipindi cha ujauzito ni vyema mjamzito kuendelea kutunza afya ya nywele zake, ngozi na hata kucha na kuzingatia mavazi yake ili aendelee kuwa na muonekano wa kuvutia.

Haya sasa niwaambie tu hii Mwananchi Scoop hasa katika kipengele cha Fashion haiachi kitu hapa tuna kudadavulia kila kitu kinachohusu mitindo na urembo kiujumla, mimi nikwambie tu bado tunakuhitaji tene next weekend kuna matamu zaidi ya haya kipenzi!!!






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Asha Charles


Latest Post