Urembo wa shanga katika nguo unavyo endelea kutamba mjini

Urembo wa shanga katika nguo unavyo endelea kutamba mjini

Enhee!! Nakusalimia kwa jina la fashion, fashion ziendelee kama kawaida ni weekend nyengine tunakutana tena hapa hapa kwaajili ya kukudadavulia yale yote yanayo happen katika mitindo mbalimbali.

Leo katika segment ya Fashion nimekusogezea kitu tofauti kidogo ambacho watu wanadhani kimepitwa na wakati basi bhana mwanetu si kingine bali ni urembo wa shanga/ stone katika nguo.

Kwanza kabisa katika jamii za Kiafrika shanga imekuwa sehemu ya urembo ikivaliwa bila kujali jinsia lakini hasa ilikuwa ikivaliwa na wanawake au wamama wa kiafrika.

Kipindi hicho baadhi ya jamii mfano koo za kichifu, machifu walikuwa wanavaa shanga shingoni, mkononi na hata miguuni yaani ilikuwa nikama tamaduni yao.

Nguo za ushanga hazipotezi upekee wake tangu enzi za mababu zetu hapo awali ushanga ulikuwa unatumika kama urembo kwa wanawake na wanaume hasa koo za kitemi.

Wabunifu wa mavazi wakapiga hatua na kuangalia namna wanavyoweza kuweka ubunifu huo washanga na kuleta mwonekano wa kipekee na unaopendeza kuliko awali.

Urembo wa shanga katika nguo za sherehe umekuwa na mvuto hasa kuleta mwonekano wa kipekee ikivaliwa nyakati za usiku.

Siku za hivi karibuni watu wengi wamekuwa wakishona nguo na kunakshia ushanga kwa juu badala ya kutumia nguo za hariri (less material) ambazo hupatikana katika maduka ya vitambaa vya nguo.

Wanamitindo wengi wa mavazi wameona njia ya kuongeza urembo wa shanga juu ya nguo umekuwa ukileta mwonekano wa kipekee, kuna njia nyingi za kuweka shanga miongoni mwa njia hizo ni njia ya kutumia gundi ya umeme (gun glue), ambapo kunakuwa na mashine ambayo hutiwa gundi inayoyekuka baada ya kuwasha umeme kwenye socket.

Njia nyingine ni kushona shanga kwa kutumia sindano ya mkono ushanga unaweza ukawekwa katika mitindo tofauti tofauti ya nguo kama blauzi, sketi na magauni ya harusi.

Mwanachi Scoop ikatupia jicho kwa mwanamitindo wa mavazi Pendo Mkonya, akieleza kuwa nguo nyingi za sherehe huwa anaweka shanga mwenyewe kwakutumia mkono na wakati mwingine mashine.

Hufanya hivyo ili kutengeneza upekee wa mavazi anayoyabuni yeye na watu wengine, pia kuweka shanga kwenye nguo huleta mwonekano mzuri anasema.

“Wateja wangu wengi wa nguo za harusi na sherehe hasa wadada huwa hawapendi nitumie hariri pekee (less material) kwa sababu hawataki wakienda kwenye sherehe kufanana na wengine,

Wanapenda upekee hivyo hunilazimu kuweka ushanga juu ya nguo na mara nyingi huwa natumia mkono kwa sababu hudai kuwa ushanga una urembo wake wa asili tofauti na vitambaa vya kawaida tu”alisema Pendo.

Hatukuishia hapo tu mpaka kwa mwanamitindo mwengine Halima Said yeye ni mbunifu wa shanga za kimasai, amesema hapo awali alikuwa akitengeneza urembo tu wa shanga kwa ajili ya jamii ya Wamasai.

Laahasha! wakati mwingine wapo waliokuwa wanahitaji kwa ajili ya kuvaa tu kuna wakati baadhi ya wabunifu wakubwa walikuwa wakimpa kazi za kutengeneza ushanga kwenye nguo.

Katika kipindi cha mwanzo alipata wakati mgumu kwa sababu hakuwahi kufanya hivyo kabla lakini kutokana na uzoefu alionao alifanya vizuri na kutoa matokeo chanya katika ubunifu wake anatueleza.

“Nilikuwa najua kuwa ushanga unaweza kuishia katika ngazi ya urembo tu kumbe hata mavazi yanaweza kuwekwa ushanga na kuvutia.

Alikuja mbunifu mmoja maarufu tu akaniambia kama ninaweza kutengeneza ushanga kwa staili hio hio kwenye nguo, mwanzo nilikataa na kuhisi hiyo nguo itakuwaje lakini nilipotengeneza nguo ilikuwa nzuri sana.” Alisema Halima.

Aidha katika upande wagharama za kuwa tengeneza urembo huo Halima anasema kuna bei tofauti tofauti inategemea na nguo anaeleza.

“Kuweka urembo katika nguo kuna gharama kidogo kwa kuwa huwa nachukua muda mrefu utengeneza ili nguo ikamilike huwa naanzi kwa bei ya shilingi lakimoja na kuendelea”alisema mwanamitindo huyo

Ukiachilia hayo kumbe unaweza ukaitoa nguo dukani ambayo haina urembo ukaenda kwa fundi akakubunia kwa njia ya vishanga kama navyo sema binti mpenda urembo Veronica Mambwe yeye hapendi kuvaa sare na mtu mwengine.

“Sipendi kuingia ukumbini kila mtu afanane na mimi, huwa namtafuta fundi atakaye niwekea urembo wa mkono ili utofautiane na ule wa dukani.” alisema Veronica.

Sasa mpenzi itoshe kusema Mwanachi scoop hakuna tunacho bakisha kama ulikuwa unajua urembo washanga umepotea, bado upo kwenye chat isipo kuwa tu hivi leo urembo huo umeboresha na kuwekwa kwenye nguo tofauti na zamani ulikuwa unavaliwa mwilini.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Asha Charles


Latest Post