Simulizi:sehemu ya 11

Simulizi:sehemu ya 11

Na Innocent Ndayanse

Alitembea harakaharaka ili kufanya dereva asione  kuwa anacheleweshwa. Dakika chache baadaye alikuwa ndani ya nyumba aliyoishi.

Huko ndani alimkuta Hilda akijishughulisha na usafi. Hakuhangaika naye, aliifuata ile saraka iliyohifadhi bastola, akaifungua. Bastola kubwa ya Kirusi G- Peacemaker -231 ikajaa kiganjani! Haraka akaifungua na kupachika zile risasi tatu alizozinunua Mwenge, kisha akatwaa shilingi 30,000 katika ile akiba yake.

Alipojitazama kidogo akajiona hayuko kamili. Akavua hii suruali nyeusi ya kitambaa chepesi na hili shati la miraba yenye mchanganyiko wa rangi nyeusi na nyeupe, badala yake akatinga suruali pana ya ‘cadet’, yenye mifuko mingi na mikubwa, shati pana na kofia ya Parma kichwani.

Akajitazama kwenye kioo na kutabasamu kidogo, akiridhishwa na mabadiliko haya. Akaipachika bastola katika mmoja wa mifuko ya suruali hiyo, mfuko ambao haikuwa rahisi kwa mtu asiyehusika kuweza kubaini chochote kuhusu silaha hiyo. Pesa zilitumbukizwa katika mfuko wa shati.

Akatoka huku akimwacha Hilda kaduwaa. Alipofika kwenye gari akafungua mlango na kuingia kisha akamtupia swali dereva: “Chaji yako ni kiasi gani?”

“Kutoka Mwenge mpaka hapa au mpaka Ubungo?”

“Mpaka Ubungo.”

Dereva alifikiri kidogo kisha akajibu kwa upole, “Tufanye arobaini tu.”

“Nitakupa thelathini.”

“Mafuta, mwanangu,” dereva alilalamika. “Mafuta yamepanda sana. Si unaona hata watu wa daladala wameshapandisha nauli zao?”

“Pamoja na hayo, tumalize biashara mimi na wewe, mambo ya daladala hayatuhusu! Mwishowe utaniambia na treni ya Mwakyembe imepandisha bei. We’ vipi msh’kaji wangu? Kama inashindikana, basi nipe chaji ya kutoka Mwenge hadi hapa, tuachane!”

Dereva alifikiri kidogo kisha akasema, “ Ok, twende.”

SAA 5 asubuhi, ndani ya chumba fulani, katika gesti –bubu eneo la Ubungo, Kipanga alikuwa ameketi kitandani huku akiwa mtupu kama alivyozaliwa. Mbele yake, stuli tatu zilikuwa zimebeba chupa kadhaa za bia. Pale kitandani alipoketi, kulia kwake alipakana na mwanamke mweupe na mwenye mwili mkubwa ambaye pia, kama Kipanga, hakuwa na vazi lolote mwilini.

Macho ya mwanamke huyo yalionyesha wazi kuwa bado ‘hajatulia,’ na vituko  alivyovifanya mwilini mwa Panja akihusisha mikono na kinywa, vilidhihirisha ni jinsi gani amekubuhu katika nyanja ya kuhudumia wanaume faragha.

Upande wa kushoto kulikuwa na mwanamke mwingine, huyo pia akiwa na ujazo wa minyama katika baadhi ya maeneo ya mwili wake, ujazo ulioweza kuyavuta macho ya mkware yeyote pale alipopita mitaani akitembea kwa madaha. Huyu pia alikuwa mtupu kama alivyozaliwa!

Wanawake hao waliingia humo chumbani asubuhi ya siku  hiyohiyo baada ya kujipitisha-pitisha nje ya gesti hiyo kwa lengo la kumnasa Kipanga.

Ni baada ya kuona kuwa huenda wangeambulia patupu, ndipo aibu zikawekwa pembeni, wakamvaa mhudumu wa gesti na kumtobolea ukweli kuwa wamesikia eti hapo kuna ‘pedeshee’ ambaye anamwaga sana pesa kwa vimwana hususan wale watakaoweza kumfanyia vimbwanga vizito vya mapenzi chumbani mithili ya waigizaji wa sinema za ngono. Wale wanawake wasiojua kuwa aibu ni mdudu wa aina gani na kinyaa ni nini.

Mhudumu naye hakuwa na hiyana, akamfuata Kipanga na kumtaarifu juu ya ujio wa wanawake hao. Kipanga angekataa? Akatae wakati usiku uliopita alilazimika kumtimua mwanamke mmoja ambaye aligoma kumhudumia ipasavyo licha ya kumpa shilingi 50,000?

“Wanalipa?” Kipanga alimuuliza mhudumu.

“Nakwambia wako bomba kishenzi, mwanangu.”

“Hawataleta za kuleta katikati ya shughuli?”

“Mi’ nawajua,” mhudumu alijibu haraka. “Ni mi-shangingi iliyobobea katika fani. Nakwambia, utaikimbia mwenyewe.”

“Poa, kailete.” 

Dakika chache baadaye ndipo wanawake hao wakajitoma chumbani humo. Naam, Kipanga akakubali kuwa ni wanawake wanaostahili kuwahudumia wanaume wenye njaa. Takriban saa nzima baada ya wanawake hao kukitekeleza kile kilichowaingiza humo chumbani, hatimaye Kipanga aliagiza tena bia na wakawa wakinywa taratibu.

Ni kipi kingine ambacho Kipanga angehitaji, zaidi ya wanawake wa aina hiyo chumbani humo? Wanawake waliokuwa radhi kumridhisha kimapenzi kwa namna yoyote aliyotaka! Nani kama yeye katika dunia hii? Ni starehe ipi duniani zaidi ya hiyo aliyopewa na warembo hao?

‘Haya ndiyo maisha,’ alijisemea kimoyomoyo huku akiwatupia macho kwa zamu wanawake hao, akivutiwa na uzuri wa maumbile yao, maumbile yaliyoichemsha damu yake kiasi cha kujikuta akitaka tena na tena, ikibidi wote kwa mkupuo, jambo lililokuwa gumu kutekelezeka

Itaendeleaa…………………………..






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Detricia Pamba

A Digital Journalist, Content Creation Executive at Mwananchi Communications Ltd and Chief Editor of Mwananchi Scoop. I'm also writes stories around Technology, every Wednesday on Mwananchi Scoop. My other famous segments on Mwananchi Scoop include LISTI and WHO’S HOT.


Latest Post