Sh2 milioni kugombaniwa kwa atakayechora picha ya kuvutia watalii

Sh2 milioni kugombaniwa kwa atakayechora picha ya kuvutia watalii

Katika kukuza sekta ya utalii Tanzania wanafunzi wa chuo kikuu cha Dar es Salaam, wanaosoma sanaa ya ubunifu pamoja na wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha sita kutoka shule mbalimbali wanashindanishwa kuchora picha zinazowakilisha vivutio vilivyo nchini.

Shindano hilo lililopewa jina la Uzuri wa Tanzania Fahari Yangu lilizinduliwa Septemba 27, na leo Septemba 30, 2024 linaendelea katika chuo kikuu cha Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari Dkt Erick Mgema, kutoka idara ya Sanaa ya Ubunifu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, amesema kila uwasilishaji utapimwa kwa maelewano ya kionyesho, ustadi wa matumizi ya vyombo vya sanaa, matumizi ya rangi na uwezo wa kushirikisha na kuvutia watazamaji.

"Washiriki wanapaswa kuchora picha zenye vigezo hivi ni pamoja na muundo na mpangilio, ujuzi wa kiufundi, rangi na toni, ubunifu na uasilia pamoja na kina cha simulizi na tafsiri ya mada",amesema Mgema.

Kwa upande wake Dkt Issa Mbura ambaye ni mhadhiri kutoka idara ya Sanaa ya Ubunifu chuoni hapo amesema washiriki wanapaswa kuchora picha zitakazoakisi uzuri wa Tanzania.

"Washiriki watanufaika na semina ya mafunzo ya siku mbili katika chuo cha wachoraji ikifuatiwa na vikao vya uchoraji vya siku 8, lakini pia washiriki watakaoingia fainali michoro yao itahukumiwa na kuonyeshwa wakati wa hafla ya utoaji wa zawadi itakayofanyika mapema Novemba mwaka huu katika Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam", amesema Dkt Mbura.

Sambamba na hilo washindi watapata zawadi mbalimbali ikiwa pamoja ni Sh2 milioni kwa wanafunzi wa vyuo vikuu, kwa wale kidato cha kwanza hadi cha sita watapatiwa kompyuta mpakato na compyuta kibao.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Christina Lucas


Latest Post