Kolabo za wasanii bongo na Marekani zinavyogeuka hewa

Kolabo za wasanii bongo na Marekani zinavyogeuka hewa

Na Aisha Charles

Hivi karibuni kumezuka mtindo wa wasanii kuonesha jumbe wanazowasiliana na wanamuziki kutoka mataifa mbalimbali hasa Marekani, wakiwa wanawaomba kufanya nao kazi. Jambo ambalo ndani yake linaonekana kuwa na uchungu tamu.

Wengi wanaamini ni njia ya kuonesha ukubwa wao kuwa wanawasiliana na wakali kutoka Mataifa mengine, huku wengine wakitumia njia hiyo kuwaweka tayari mashabiki wao.

Huenda wote wakawa sahihi lakini shida huanzia pale ambapo kolabo hizo kutofanyika, jambo ambalo limekuwa likivunja imani ya mashabiki kwa wasanii wao.

Hivi karibuni msanii Harmonize alionesha maongezi yake na rapa Meek Mill kutoka Marekani akiwa anamuomba kolabo lakini msanii huyo alionekana kutomtambua kabisa Konde Boy licha ya kuwa tayari amefanya ngoma kadhaa ambazo zimekuwa zikifanya vizuri.

Mbali na hilo Harmonize aliwahi kudokeza kufanya ngoma na rapa wa Marekani Nick Minaj lakini hadi leo ngoma hiyo haijasikika mahali popote.

June mwaka huu mwanamuziki wa hip-hop Roma Mkatoliki alionesha mawasiliani yake na rapa wa Marekani Jada Kiss akimuomba kushirikiana kwenye ngoma.

Diamond aliwahi kudokeza kuwa atatoa album ya Swahili Nation ambayo itakuwa na kolabo na wanamuziki kama Busta Rhymes, Wiz Khalifa, Snoop Doggy, na Swizz Beatz lakini hadi sasa bado mashabiki wake hawajasikia chochote licha ya kwamba alionekana Studio akiwa na Swizz na Busta.

Mwaka 2017 Diamond pia aliwahi kutoa dokezo yuko mbioni kufanya kazi na Chris Brown ambayo hadi sasa hawajafanikiwa kufanya.

Shida siyo kuomba kolabo hizo bali, mazoea ya kuwaweka tayari mashabiki kwa ujio wa kazi ambazo hazifanyiki ndiyo doa kwenye kiwanda cha muziki Bongo, hupelekea mashabiki kuvunja imani kwa wasanii wao kwa sababu hata ukimya wa kolabo hizo huishia hewani bila ya mashabiki kupewa mrejesho wowote.

Kutokana na michezo hiyo ya wasanii kuahidi na kuomba kolabo ambazo mwisho huyeyuka hewani wadai mbalimbali wa muziki wametoa mitazamo yao juu ya suala hilo.

Mdau wa muziki nchini Maulidi Masoud, mkazi wa Tabata, Dar es Salaam ameeleza kuwa wasanii wa Bongo bado hawajafikia kufanya kazi na wasanii kama Chris Brown huku akidai kuwa levo zao bado ni za wanamuziki wa Afrika Mashariki.

“Wasani wa Kibongo bado sana ila wanalazimisha kufanya kazi na wasanii wa Marekani kama Chris Brown siyo mchezo ujue wao wajikite kwanza kufanya kazi na Wanigeria na wasanii wa karibu pia wapunguze kuiga kwa sababu vipaji wanavyo unakuta mwanamuziki anaiga hadi kuvuta sigara ili afanane na Wamarekani.” ameseama.

Aidha mdau mwingine wa muziki Juster Charles mkazi wa Kigogo amesema kuwa kutamani kwao kufanya kazi na wasanii wa kimataifa kunawafanya waendane na muziki wa sasa unavyotaka kuanzia miondoko na midundo.
.
.
.
#MwananchiScoo
#BurudikaNasi






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Asha Charles


Latest Post