Dk Malale:  wanaopunguza mwili kwa kuacha kula baadhi ya vyakula wako hatarini kupata tatizo la akili

Dk Malale: wanaopunguza mwili kwa kuacha kula baadhi ya vyakula wako hatarini kupata tatizo la akili

Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Dunia (WHO) zinaonesha kuwa takribani watu bilioni 1 duniani kote wanaishi na matatizo ya akili.

Takwimu hizo ambazo zilitolewa mwaka 2020 zinaonesha kuwa moja ya visababishi vya tatizo la akili ni umaskini uliokithiri, kutengwa na jamii, kuwa tegemezi, upweke, upotevu wa vitu mbalimbali.

Visababishi vingine ni matatizo ya mahusiano, kukosa huduma muhimu, mafarakano, unyanyapaa, unyanyasaji na ubaguzi wa aina mbalimbali.

Hata hivyo inaelezwa kuwa ipo sababu nyingine inayosababisha mtu kupata tatizo la akili ambayo ni mtu kupunguza mwili kwa kuacha kula baadhi ya vyakula.

Katika siku za hivi karibuni, kumekuwa na harakati zinazofanywa sehemu mbalimbali, hasa katika mitandao ya kijamii, kuhamasisha watu kupunguza mwili na uuzwaji wa dawa tofauti zinazodaiwa kusaidia tatizo hilo.

Dk. Charles Malala ni Mratibu wa Lishe Manispaa ya Temeke anafunguka na kusema wanaopunguza mwili kwa kuacha kula baadhi ya vyakula (diet) wapo hatarini kupata madhara ya kuwa dhaifu kiakili na kuandamwa na maradhi.

Alisema ili ubongo wa binadamu ufanye kazi unahitaji kupata glucose ya kutosha ambayo inapatikana kwenye vyakula vyenye utajiri wa wanga ambavyo ni nafaka, mizizi pamoja na ndizi mbichi.

“Kwenye nafaka tuna mahindi, mtama, ulezi, uwele, ngano, mchele vyote hivi ni vyakula ambavyo vinazalisha wanga, hivyo hichi kirutubisho kinachoitwa wanga ndicho chanzo cha upatikanaji wa glucose katika mwili wa binadamu.

“Na glucose hii inahitajika kwa wingi sana katika mwili wa binadamu ili ubongo uweze kufanya kazi, sasa mtu anapofanya zoezi la kupunguza uzito au mwili wa kuacha kula vyakula vya wanga uwa anasababisha ubongo kukosa hiyo glucose ya kutosha hivyo anaweza kupata matatizo ya akili,” alisema

Alisema ubongo ukikosa glucose ya kutosha unapoteza uwezo wa kufanya kazi yake ya kuongoza mwili wa binadamu kufanya mambo mbalimbali ikiwemo kutunza kumbukumbu.

Dk. Malale alisema vyakula vyenye mafuta ni muhimu katika mwili wa binadamu kwa sababu usaidia uyejushaji wa vitamin mbalimbali vinavyohitajika katika mwili hivyo mtu anapoacha kula mafuta kwa kisingizio cha kupunguza mwili kunasababisha baadhi ya madini na vitamin kushindwa kusafiri mwilini.

“Ukiangalia mfano Vitamin A, D, K na E vitashindwa kusafirishwa ndani ya mwili kwa sababu ya ukosefu wa mafuta kwahiyo unakuta vitamin hivi kutofyonzwa vizuri kutokana na ukosefu wa mafuta ndani ya mwili na usababisha ubongo kushindwa kufanya kazi vizuri,” alisema

Dk. Malale anafafanua kuwa ili mtu ubongo wake uweze kufanya kazi vizuri na asipate tatizo la akili ni lazima apate mlo kamili utakaowezesha idara mbalimbali katika mwili wake ziweze kufanya kazi pia.

“Tukumbuke kuwa vyakula tunavyokula vinategemeana mtu ukiacha kula vyakula vyenye mafuta tambua kuwa kuna baadhi ya vitamin vitashindwa kufyonzwa ndani ya mwili na kukosa baadhi ya vitamin hivyo kusababisha mtu kupata matatizo ya akili,” alisema

Alisema kwenye vyakula vya wanga yapo madini yanayopatikana, mtu akikosa kula hatopata virutubisho na vinasababisha tatizo la akili.

“Sio sahihi mtu kupunguza mwili kwa kuacha kula baadhi ya vyakula, kitu anachopaswa kufanya katika hilo kwanza kujua sababu kwa nini una uzito mkubwa kwani ukilitambua hilo inakuwa ni rahisi sana kuupunguza,” alisema

Aidha Dk. Malale amesisitiza kuwa suala la uzito kuwa mkubwa si tatizo ila litakuja kuwa shida kama mtu akianza kuumwa miguu kwa sababu ya uzito huo.

“Lakini kama uzito mkubwa haumsababishii mtu ugonjwa wowote ulazimiki kuupunguza kwa kuacha kula baadhi ya chakula zipo mbinu mtu anaweza kufanya,” alisema

Anachopaswa mtu kufanya ili kupunguza mwili….

Alisema moja ya jambo ambalo mtu anapaswa kulifanya ili kupunguza mwili ni kubalansi mlo yaani kula mlo kamili na kujiepusha na kuacha kula baadhi ya vyakula kwa kisingizio cha kupungua.

“Mtu ili asipate tatizo la akili asiache kula vyakula vya mafuta, wanga na vingine kwa ujumla, ila anatakiwa kufanya mazoezi  mara kwa mara,” alisema






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm


Latest Post