Chid Benz: Natembea kwa miguu, madereva wananiogopa

Chid Benz: Natembea kwa miguu, madereva wananiogopa

Msanii wa Hip Hop, Chid Benz amesema ameamua kutembea kwa miguu kutokana na madereva wengi wa bodaboda kuogopa kumbeba wakidhani hatawalipa nauli zao.

Chid ambaye aliwahi kutamba na nyimbo kama Dar es Salaam Stand Up, Hasira za Nini, Mpaka Kuchee na nyingine nyingi, maisha yake yamebadilika na mwenyewe amesema anapenda anavyoishi sasa na hata akiwa na hela hatayabadilisha.

Mwananchi Scoop ilikutana na Chid akiwa kwenye kibanda cha kuuza mihogo ya kukaanga Sinza, Kijiweni, Dar es Salaam akisubiri kupata huduma hiyo na kufunguka usafiri wake mkubwa ni miguu yake haogopi watu wala waandishi na anapenda kuishi maisha ya kawaida.

"Maisha ninayoishi sasa hivi ni mazuri sana, si unaona hapa nasubiria mihogo ya kukaanga, lakini watu wananipita tu hawanishangai, yaani siishi kwa uoga sababu ya watu watanionaje au waandishi wa habari  wataniona.

"Haya ndiyo maisha ninayoishi na hata nikija kupata pesa niteendelea kuishi hivi, ila kuna hawa waendesha bodaboda huwa wanazingua sana, yaani nikiwasimamisha kutaka usafiri baadhi yao wanakataa kunipandisha wanadhani sitawalipa pesa," amesema na kuongeza ana uwezo wa kutembea kwa miguu kutoka Sinza hadi Magomeni bila ya kupata usumbufu wowote na maisha yake yote sasa hivi asilimia kubwa anatembea kwa miguu.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Christina Lucas


Latest Post