Stephen Curry anavyoupiga mwingi kupata fursa, Kupitia mpira wa kikapu

Stephen Curry anavyoupiga mwingi kupata fursa, Kupitia mpira wa kikapu

Na Aisha Charles

Naam! watu wangu kwa mara nyingine tena katika burudani tumekutana kupashana habari zinazobamba kwenye upande huu, leo tutamzungumzia mchezaji wa mpira wa kikapu Stephen Curry, mafanikio yake  na anavyoendelea kupata fursa kupitia mchezo huo.
Miaka miwili mfululizo mchezaji wa mpira wa kikapu wa NBA kutoka nchini Marekani Stephen Curry anayeichezea ‘timu’ ya Golden State Worriors ameingia kwenye ‘rekodi’ ya kuwa mchezaji aliyepata pesa nyingi zaidi kupitia mshahara wake.

 Mwaka 2022, alizidiwa kidogo na Kevin Durant ambaye ndiye alipata pesa nyingi kutokana na ‘madili’ ya nje ya uwanja. Lakini mwaka 2023 hadi mwaka huu 2024 Curry  amesimama tena kileleni kwa kupata maokoto mengi zaidi kupitia mikataba ya matangazo mbalimbali anayopata.

 Anapigaje pesa?

Bado ameendelea kuwepo kwenye 10 bora ya wanamichezo wanaolipwa zaidi duniani, mwaka 2023 alishika nafasi ya nane akiwa amepata jumla ya  dola 103 milioni,  ambapo dola 51 milioni alizipata kwenye mshahara wake ambao ndiyo mshahara mkubwa zaidi kuwahi kulipwa kwa mchezaji wa NBA huku dola 52 milioni akizipata kwenye madili mengine ya nje ya uwanja.

Kwa sasa ‘amesaini’ mkataba mpya na team ya Golden state ambao utamuwezesha kupata dola 215 milioni ndani ya miaka minne ambapo kwa miaka mitatu ya kwanza alipata  dola 48 milioni, msimu  wa mwaka 2023-24 amepata dola 51.9 miloni, msimu huu wa mwaka 2024 -25 atapata dola 55.7 milioni.

Kwenye sekta ya mikataba mingine minono nje ya kikapu mchezaji huyo ni balozi wa Under Armour tangu mwaka 2013 na mwaka  2017 alirefusha mkataba nao ambao hadi sasa unampa zaidi ya dola 10 milioni kila mwaka.

Mwaka 2015 pia alisaini mkataba wa ubalozi na kampuni iitwayo  Brita, pia anaubalozi wa kampuni za  Unilever Degree,  JPMorgan Chase, Palm, CarMax, Callaway Golf, 2K Sports, na  Rakuten zote hizi zinampa zaidi ya dola 30 milioni kila mwaka.

Ukiachana na madili hayo ya ubalozi fundi huyu wa mpira wa kikapu pia anatumia pesa zake kuwekeza na kununua hisa kwenye makampuni mbalimbali amekuwa akipata faida ya zaidi ya dola 5 milioni kwa mwaka.

 Nyumba anazomiliki

Anamiliki mjengo unaokadiriwa kuwa na thamani ya dola 50 milioni uliopo Malibu, California, tangu  April 2021.

Nyumba hiyo ya kifahari ndani yake kuna bwawa kubwa la kuogelea, ukumbi wa sinema na sehemu ya kuchezea kikapu.

Pia ana nyumba nyingine inayopatikana Atherton, Menlo Park, California ambayo aliripotiwa kuwa yuko mbioni kuiuza.

Pia nyumba yake nyingine yenye thamani kubwa ni ile ya  San Francisco aliyoinunua kwa dola 8 milioni.

Magari anayo miliki

 

Mercedes-Benz G55- dola  156,450.

Tesla Model X 90D- dola 93,500

Infiniti Q50- dola 42,100

Porsche 911 GT3 RS- dola  416,500

Kia Sorento- dola 39,190

Range Rover Sport LWB - dola 211,000.

Cadillac Escalade ESV- dola 79,295

Porsche Panamera Turbo S - dola 190,200

 

 

Msaada anaotoa katika jamii

Ni balozi wa kampeni mbalimbali za kusaidia jamii kama Animal Rescue Foundation, Boys & Girls Clubs of America, Brotherhood Crusade, Eat. Learn. Play. Foundation.

Pia kuna taasisi kubwa ambazo zinamtumia kama balozi wao ambazo ni   United Nations Foundation, V Foundation for Cancer Research NBA Cares, Nothing But Nets, Partnership for a Healthier America,

Amewahi kuchangia dola 100,000 kwa shule moja  iliyopo Ohio ambazo zilitumika kununua vifaa na kulipa makocha wa kufundisha mpira wa kikapu.

 

Bata na uhusiano
Yupo kwenye ndoa tangu mwaka 2011 na mrembo muigizaji Ayesha Curry ambaye wamefanikiwa kupata watoto watatu ambao ni  Riley Elizabeth Curry, Ryan Carson Curry na Canon W. Jack Curry.

Kwa mantiki hiyo mwanetu wa nguvu wa Magazine yetu pendwa ya Mwananchi Scoop, kupitia mchezaji huyo wa kikapu unaweza ukahamasika kama ulikuwa na ndoto ya kuwa mwanamichezo unaweza kupata fursa nyingi kuna msemo usemao safari moja huanzisha nyingine.
.
.
.
#MwananchiScoop
#BurudikaNasi






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Asha Charles


Latest Post