Wafahamu Wahindi wenye ngozi nyeusi na nywele ngumu

Wafahamu Wahindi wenye ngozi nyeusi na nywele ngumu

Duniani kuna watu wa kila aina ambao hutoka mataifa mbalimbali, na wakati mwingine ni rahisi kugundua kuwa huyu ni wa taifa fulani kutokana na muonekano wake, bila kusahau utani ambao huwa unajitokeza kutokana na muonekano wa watu wa taifa fulani.

Wengi ukiwaambia kuhusu bara la Afrika basi hudhani kuwa watu wote waliopo Afrika ni wenye ngozi nyeusi bila kufahamu kuwa Afrika nako kuna watu wenye ngozi nyeupe, nywele nyingi laini na ndefu, ndivyo hivyo pia katika mabara mengine ambayo watu hudhani watu wapatikanao huko wote ni weupe, hivi umewahi kufahamu kuwa India kuna watu weusi na wenye nywele ngumu?

Kama bado leo hii wafahamu watu weusi wenye nywele ngumu wapatikanao India ambao laiti kama ukimuweka mmoja katikati ya mkusanyiko wa watu Kariakoo, na ukaambiwa useme yupi ni muhindi hakika utapata ugumu kwenye kumtambua.

Watu hao ni jamii ya Jarawa ambao hupatikana Kusini mwa  Visiwa vya Andaman nchini India, jamii ya watu hawa huwa na tabia ya kuhamahama kwa ajili ya kutafuta chakula na mara nyingi hupendelea kutembea katika vikundi ya watu 40 hadi 50.

Hupendelea sana kula samaki, nguruwe, kaa, asali, matunda na mizizi kwani ndio chakula chao kikuu ambacho hutumia muda mwingi kukitafuta, mgawanyiko wa kazi katika jamii ya watu hawa wameuzingatia sana wanawake na wanaume hujumuika kwenye kukusanya asali lakini kwa kazi nyingine kama vile za uwindaji wanaume huusika kwa kiwango kikubwa.

Jarawa hutumia silaha kama vile pinde na mishale ambayo huingia nazo kwenye miamba ya matumbawe kwa ajili ya kutafuta kaa na samaki wengine, pinde hizo watumiazo zimetengenezwa kwa mbao za chooi, ambazo hazipatikani katika maeneo yao hivyo mara nyingi hulazimika kusafiri umbali mrefu hadi Kisiwa cha Baratang ili kuzichukua.

Inaelezwa kuwa Mnamo 1998, Jarawa wachache walianza kuibuka kutoka msituni kwa mara ya kwanza bila pinde na mishale na kutembelea miji na makazi yaliyopo karibu, hadi hivi sasa wapo wachache waliosogea katika makazi ya watu wa jamii nyingine na wengine wanaendelea kukaa katika misuti.

#MwananchiScoop

#MwananchiForum

#Empoweringthenation






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Asha Charles


Latest Post