Kupenda kupita kiasi ni tatizo la Homoni sehemu ya pili

Kupenda kupita kiasi ni tatizo la Homoni sehemu ya pili

Inaendelea kutoka wiki iliyopita…

Inaanzaje?

Watu wawili hupendana. Kama nilivyosema, kupendana huku husababisha homoni hii kuzalishwa ubongoni. Kuzalishwa kwa kemikali hii ndiko ambako humfanya mtu aliyependa kuwa katika raha fulani isiyoelezeka. Kama ilivyo kwa mlevi wa pombe au madawa ya kulevya, kuna wakati kiwango cha nishai hushuka ambapo inabidi avute au kunywa tena. Kwa mtu aliyependa naye, kuna wakati hali ya raha hii hushuka, kutegemea mazingira.

Lakini kama wapendanao wamekutana kimwili na kukutana huko kukawapa raha kubwa sana, uwezekano wa kemikali hii kuizinga akili moja kwa moja ni mkubwa sana. Akili inapozingwa na homoni hii, mpendaji kamwe hataacha tena kumpenda huyo mtu wake.

Inakuwa kama mlevi sugu anavyotegemea pombe au madawa kupata raha ya maisha, huyu mpendaji naye atakuwa hajisikii raha bila kuwa na huyo mpenziwe, bila kujali visa na vibweka anavyomfanyia. Hata kama hashiriki naye tendo la ndoa, bado atakuwa anajisikia raha tu kuwa naye.

Msomi mmoja wa chuo kikuu cha Guelph huko Canada, George Bubenik anakiri kuwepo kwa hali hii na anasema ndio maana unaweza kukuta mtu akiishi kwenye ndoa ya mashaka na vurugu huku huku wengine wakishangaa na kutoelewa sababu. “Mtu ambaye anafurahia sana tendo la ndoa mwanzoni mwa uhusiano na mwenzake anaweza kung’ang’ania kwenye ndoa hata kama imejaa vurugu”

Anasema watu hawa wangetarajiwa kuondoka au kuzikimbia ndoa za aina hii lakini huwa hawafanyi hivyo kwa sababu wamepata usugu wa kiakili kwa zile hisia wanazozipata wakati waliposhiriki tendo la ndoa na wapenzi wao. Kama mlevi sugu wa pombe asivyoweza kuacha pombe hata kama inakaribia kumuuwa, ndivyo inavyokuwa kwa watu wa aina hii.

Haina maana kwamba hao wapenzi wao ni watu wenye kujua sana mapenzi, hapana. Ni kwamba siku ya kwanza walipokutana, ubongo ulizalisha homoni kwa wingi na ikawa imeizinga akili. Kinachojirudia hapa ni zile hisia za awali. Sawa kabisa na mlevi sugu, ambaye anaweza kuwa anakunywa pombe kali na isiyo na utamu, kwa sababu anachohitaji siyo ladha ya pombe, bali zile hisia wakati au baada ya kunywa. Hapa mwanamke au mwanaume aliye katika hilo penzi anaendeshwa na hisia anazozipata wakati wa tendo la ndoa, ambazo zimeganda akilini kupitia homoni hii ya dopamine.

Huwa hakuna kulogwa wala limbwata au mapenzi motomoto, hapana, hapa kuna tatizo la utegemezi. Mhusika ni mtu ambaye inabidi asaidiwe kama anavyosaidiwa mlevi sugu. Wengi wetu huwalaumu watu hawa au wapenzi wao, jambo ambalo bila shaka siyo haki.

Tumeshawahi kusikia bila shaka watu wakisema, ‘wewe hujui ni kwa nini anang’ang’ania uhusiano ule, anajua mwenyewe anachokipata’. Wengi wanaposema hivyo wana maana ya kile mtu huyo king’ang’anizi anachokipata hadi kutokuwa tayari kuvunja uhusiano na mpenzi anayemtesa au kumdhalilisha. Mara nyingi wana maana ya mapenzi motomoto ya kitandani. Huu siyo ukweli hata kidogo, kwani unaweza kukuta hata mapenzi ya kitandani mtu huyo hapati. Anachokipata hapa ni ridhiko linalotokana na dopamine iliyozinga ubongoni mwake.

Inakuwaje ikibidi uhusiano huo ufe:

Kuna wakati kwa sababu ya mazingira fulani fulani inabidi uhusiano huu ufe, hata kama mmoja ni king’ang’anizi vipi. Hilo linapotokea yule king’ang’anizi hukabiliwa na athari za matokeo kama vile wasiwasi, aina ya hamu ya mapenzi au kupendwa isiyoweza kuridhishwa, huzuni na hasira. Hali hizi pia huwa zinapatikana kwa mlevi au mvutaji sugu ambaye anajaribu kuacha kuvuta au kunywa.

Kuthibitisha hii Bubenik aliwafanyia utafiti panya wadogo wa porini na kugundua kwamba wanyama hawa wakizuiwa wasitoe homoni iitwayo oxytocin (sawa na homoni ya dopamine kwa binadamu) wakati wakipandana huwa hawadumu pamoja. Lakini pale wanapoachiwa watoe hiyo homoni huwa hawaachani hadi kufa.

Tunaweza kusema mtu kushikwa au kunaswa kwenye mapenzi ni suala ambalo hakuna mtu anayeweza kudai kwamba anaweza kulizuia. Kulizuia kunawezekana kama mtu ataamua kuachana na tabia ya uzinzi tu, kwani hatafikia mahali ambapo akili yake itazingwa na homoni hii.

 






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Shaban Kaluse

A Sales and Marketing in the hospitality Industry and also a freelance journalist, writing about love and relationships and educative articles which aims for youths, every Tuesday on Mwananchi Scoop.


Latest Post