Jinsi ya kupika maandazi ya nazi kwa ajili ya biashara

Jinsi ya kupika maandazi ya nazi kwa ajili ya biashara

Eeeeeeeh! Mwamba huyu hapa, I hope mko good watu wangu wa nguvu, sasa leo bwana tuko na kitu najua sio kigeni sana ila kuna baadhi ya watu kinawasumbua kutengeneza au kupika.

Kama kawaida waswahili wanasema mchele mmoja mapishi tofauti ndio kama ilivyo katika maandazi ngano moja lakini kila mtu anaupikanaji wake wa maandazi, na kama tunavyojua ngano inamapishi mengi haswaaah.

Leo utajifunza jinsi ya kutengeneza mandazi na kama ijulikanavyo chakula hiki ni moja ya vitafunwa bora kabisa wakati wa asubuhi na watu wengi hupendelea kula, hii ni kutokana na ladha yake tamu na nzuri ambayo haikinaishi kama vyakula vingine vinavyoliwa asubuhi.

MAHITAJI

  • Unga wa ngano nusu
  • Sukari glasi ndogo nusu (1 ikiwa wewe ni mpenzi wa sukari)
  • Chumvi robo kijiko cha chai
  • Iliki punje 10 hivi
  • Samli kijiko 1
  • Tui la nazi glasi ndogo 2
  • Hamira vijiko 2 vya chakula
  • Baking powder kijiko 1
  • Mafuta ya kupikia nusu lita

MAELEKEZO

Step 1: Chekecha unga kwa kutumia chungio kwenye chombo utacho kandia unga wako.

Step 2: Chukua kikombe weka hamira, sukari vijiko 2, unga vijiko 2 na iache kwa dakika 5 mpaka ifure (iumuke).

Step 3: Chukua unga ulio uweka kwenye chombo chako, weka baking powder, chumvi, sukari na hiliki kisha changanya vizuri.

Step 4: Chukua hamira iliyoumuka changanya na unga wako kisha weka tui lako kidogo kidogo na uanze kuukanda.

Step 5: Kanda unga wako kwa dakika 10 mpaka uwe laini kisha uuache kwa muda wa dakika 5.

Step 6: Ongeza samli na uendelee kuukanda unga kisha uweke kwenye bakuli na uufunike ili usipitishe hewa uache tena kwa muda wa dakika 10.

Step 7: Ukishaumuka kata madonge na uyasukume kwa kutumia unga mkavu upate duara kubwa kama chapati hivi, ila isiwe nene sana wala nyembamba sana.

Step 8: Kisha kata mandazi yako kwa umbo la pembe tatu ama upendavyo na yaache mandazi yako yaumuke kwa dakika zisizopungua 10 hivi.

Mimina mafuta kwenye karai yaache yapate moto kiasi kisha anza kuweka vipande vyako hatua kwa hatua, hakikisha mandazi hayawi mengi kwenye karai ili yaachane na uweze kuyageuza kwa urahisi.

Ili andazi liumuke vizuri wakati lipo katika karai, limwagie mafuta juu kwa kutumia mwiko wako, alafu ndio uligeuze baada ya kuumuka vizuri.

Andazi likiiva epua weka kwenye chujio au shashi kulichuja mafuta ya ziada, Likipoa tayari kwa kula kwa chai, mchuzi wa nyama yoyote ile, mbaazi, maharage n.k.

Haya dhumuni letu sisi ni biashara so sheria ni ile ile kama hujawahi kupika maandazi usikurupuke please anza kwa kujifunza ndo maana nimeweka unga nusu hapo juu nikimaaniasha wa kuanzia kujifunza, ukiona sasa umeweza basi unatengeneza kwa ajili ya biashara, na uzuri wa haya unaweka hata kwenye kibaraza cha nyumba yako nje na ukapata wateja. So wakati ni wako amka acha kuwa beki tatu wewe.

 






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post