Imetimia miaka 17 tangu Jay Z, 55, na Beyonce Knowles, 43, kufunga ndoa Aprili 4, 2008, hadi sasa harusi yao ni moja ya mambo yanayojadiliwa sana kutoka katika familia hiyo ya The Carters kutokana na jinsi walivyotekeleza jambo hilo.
Uhusiano wao ulianza mwishoni mwa miaka 1990 ila walipotoa kolabo yao wa kwanza, 03 Bonnie & Clyde (2002) iliyosampo wimbo wa 2Pac, Me and My Girlfriend (1996), ndipo tetesi za kuwa pamoja zilishika kasi ingawa walikanusha wakati huo.
Beyonce ambaye awali alivuma na kundi la Destiny’s Child, alisema alikutana na Jay Z akiwa na umri wa miaka 18 na mwaka mmoja baadaye wakaanzisha uhusiano ila kuhusu ni wapi walipokutana kwa mara ya kwanza imebaki kuwa siri yao.
Mnamo Novemba 2006 Beyonce, mshindi wa Grammy 35 akiongea na Jarida la Cosmopolitan alisema katika maisha yake hajawahi kujiona kama Bibi harusi ingawa aliwahi kufikiri kuhusu aina ya harusi anayoitaka ambayo sio kubwa.
Ndivyo ilivyokuwa, harusi yao waliifanya kwa faragha huku ikiwa na wageni takribani 40, miongoni mastaa walioalikwa ni wasanii wa Destiny’s Child, Kelly Rowland na Michelle Williams, pamoja na marafiki zao, Gwyneth Paltrow na Chris Martin.
Pia walijumuika na wanafamilia kadhaa wakiwemo wazazi wa Beyonce, Matthew na Tina pamoja na mdogo wake Solange, vilevile mama yake Jay Z, Gloria Carter, bibi, dada na mpwa wake walihudhuria.
Kulikuwa na mavazi ambayo wageni walipaswa kuvaa, wanawake walivalia nguo nyeupe huku wanaume wakivaa nyeusi. Kubwa zaidi simu zote za wageni zilikusanywa kabla ya shughuli kuanza ili kuhakikisha hakuna anayepiga picha wala kuchukua video.
Tarehe yao ya kufunga ndoa, yaani Aprili 4 ilikuwa na maana kubwa kwao na muhimu kwa sababu wana uhusiano wa karibu na namba 4, uhusiano huo unakuja kwa maana Beyonce alizaliwa Septemba 4 huku Jay Z ikiwa ni Desemba 4.
Kutokana na hilo, badala ya kuvishana pete, wote wawili walichora tattoo yenye alama ya nne (4:4) katika vidole vyao vya pete lengo likiwa ni kuonyesha kuheshimu namba hiyo ambayo wanaitaja kama ya bahati katika maisha yao.
Katika hafla ya tuzo za MTV VMAs 2011, wakati Beyonce akitumbuiza wimbo wake, Love On Top (2011) alitangaza kuwa ana ujauzito wa mtoto wao wa kwanza, na kufikia Januari 7, 2012 akajifungua mtoto wa kike ambaye alipewa jina la Blue Ivy Carter.
Juni 13, 2017 familia yao iliongezeka baada ya Beyonce kujifunga watoto pacha, Rumi na Sir Carter. Rumi ni wa kike na amekuwa akionekana na wazazi wake mara kwa mara katika mitoko yao ila huyo wa kiume, Sir huwa anafichwa sana mbele ya macho ya umma.
Jambo moja la kukumbukwa katika harusi hiyo ilikuwa ya faragaha zaidi, wageni waalikwa hawakuruhusiwa kuingia na simu na baadaye mastaa hao walikataa ofa ya Dola 11 milioni kutoka kwa majarida makubwa ambayo walitaka picha zao kwa sababu za kibiashara. Hata hivyo baadhi ya tetesi zinadai kuwa ndoa ya wawili hao imeshavunjika lakini hakuna uthibitisho wa hilo.

Leave a Reply