Mastaa waliowatoa wenzao kimuziki Bongo

Mastaa waliowatoa wenzao kimuziki Bongo

Peter Akaro

Imekuwa kawaida katika siasa, biashara, michezo, muziki, filamu na mitindo, kila anayefanya vizuri upande huo, kuna mtu alimshika mkono au kumvutia kufanya mojawapo kati hayo machache.

Je, kwenye muziki wa Bongofleva hali ipo hivi?, wasanii wamekuwa wakishirikisha kwenye nyimbo kila siku lakini kuna wale kufanya hivyo kulipelekea kuleta au kutengeneza majina mapya na baadaye kuwa makubwa kwenye muziki huo kama ifuatavyo.

1. Alikiba > Ommy Dimpoz

Wawili hawa walikutana G Records, kisha prodyuza KTG akawatengenezea mdundo wa wimbo, Nai Nai (2011) ambao Ommy Dimpoz alimshirikisha Alikiba, baada ya hapo jina la Ommy likawa maarufu kila kona.

Kufanya vizuri kwa wimbo huo kulipelekea Dimpoz kushinda tuzo mbili za muziki Tanzania (TMA) 2012 kama Msanii Bora Chipukizi na Wimbo Bora wa Kushirikina, kipengele alichokuja kushida tena kupitia wimbo, Me and You (2012) akiwa na Vanessa Mdee.

2. Belle 9 > Young Killer

Rapa Young Killer alivuma baada ya kutoa ngoma yake, Dear Gambe (2013) akimshirikisha Belle 9, pia ngoma hii ilimpatia tuzo ya TMA kama Msanii Bora Chipukizi 2014, na tangu hapo hajawahi kushinda tuzo hiyo tena.

Kabla ya wimbo huo, Young Killer aliyekuwa akisifika kwa kuandika mistari kwenzi na kuichana, tayari alikuwa amesharekodi baadhi ya nyimbo kama Winner (2010) uliotayarishwa na Duke Tachez na Deey Classic huku akimshirikisha Barakah The Prince

3. Mwana FA > Maua Sama

Baada ya kumaliza kurekodi wimbo wake, So Crazy (2013), Maua Sama kupitia rafiki yake aliwatumia wasanii kama Alikiba, Ommy Dimpoz na Ben Pol ila ni Mwana FA pekee aliouelewa, ndipo wakarudia kuurekodi na alipotoka ukamtambulisha Maua Sama.

Hata hivyo, Maua Sama alikuwa amesharekodi wimbo huo huko nyumbani kwao Moshi ila alipokuja Dar es Salaam na kukutana na Mwana FA, waliamua kwenda kuurudia kwa Marco Chali, mshindi wa TMA kama Mtayarishaji Bora 2008.

4. Belle 9 > Shetta

Kutoka kuwa dansa wa Dully Sykes chini ya Misifa Camp hadi kuwa rapa ilikuwa ni kujitafuta kwa Shetta ila baada ya kuachia wimbo wake, Nimechokwa (2011) akimshirikisha Belle 9 ndipo akatoka rasmi kimuziki.

Ikumbukwe kwa mara ya kwanza Shetta alirekodi studio kwa Miikka Mwamba, wakati huo alikuwa darasa la nne na mtu aliyemsaidia hadi kumudu gharama za kurekodi ni Ali Choki ambaye alijitolea kumsimamia kimuziki ila hakuweza kutoka wakato huo.

5. Ben Pol > Darassa

Hakuna ubishi kuwa wimbo, Sikati Tamaa (2012) ambao Darassa kamshirikisha Ben Pol ndio uliomtoa kimuziki licha ya huko nyuma kurekodi nyimbo kibao ila huu hadi sasa una heshima yake kwa wengi huku akiachia remix yake akiwa na Godzilla na Joh Makini.

Na ilimchukua miaka zaidi ya mitatu kutengeneza ngoma nyingine kubwa kama hiyo, nayo ni Muziki (2016) akimshirikisha Ben Pol tena, na hadi sasa hakuna ngoma ya Darassa iliyouza zaidi katika majukwaa ya kidigitali kama hii.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Christina Lucas


Latest Post

Latest Tags