Mwanamuziki wa Bongo Fleva nchini Yammi ameweka wazi kuwa amelipa kiasi cha Sh100 milioni kuondoka katika lebo ya ‘The African Princess’ inayomilikiwa na msanii Nandy.
Yammi ameyasema hayo wakati wa uzinduzi wa wimbo wake wa ‘Raha’ usiku wa kuamkia leo Juni 5,2025 huku akieleza kuwa awali Nandy alihitaji pesa nyingi lakini baada ya kukaa na kuzungumza ndipo wakafikia makubaliano hayo.
“Sijalipiwa na lebo yoyote wala menejimenti, kwenye maisha hapa kuna watu wengi wana roho nzuri sana wasamalia wema, kila mtu anadesten helper wake, ni mtu tuu aliona mimi ni mtoto mzuri nina tabia nzuri namfurahisha mpole akaamua anisaidie.
Alilipia Sh100 milioni, ilikuwa ni zaidi ya hapo lakini baada ya kuongea naye kama dada akapunguza,”amesema Yammi
Ikumbukwe lebo ya Nandy ilitangaza kutemana na msanii huyo mwezi Mei mwaka huu, ambapo aliingia katika lebo hiyo Januari 20, 2023.
Yammi alisaini mkataba na The African Princess baada ya Nandy kuvutiwa na video zake za uimbaji kwenye TikTok. Baada ya kusainiwa, alitoa EP yake ya kwanza yenye nyimbo tatu ambazo ni Namchukia, Tunapendezana, na Hanipendi, ambazo zilipokelewa vyema na mashabiki.
Katika kipindi chote akiwa chini ya lebo hiyo, Yammi alifanikiwa kujizolea umaarufu mkubwa, akiwa miongoni mwa wasanii wa kike waliopata streams nyingi zaidi kwenye Boomplay mwaka 2023, huku akitanguliwa na Zuchu na Nandy.

Leave a Reply