
Kesi ya P Diddy yazidi kumwelemea, mlinzi wa hoteli atoa ushahidi
Ni wiki tatu mfululizo kesi ya Sean "Diddy" Combs inaendelea kusikilizwa mahakamani. Hatimaye shahidi mwingine Eddy Garcia, aliyekuwa mlinzi wa usalama wa hoteli ya InterContinental mjini Los Angeles alipanda kizimbani, akiweka wazi kuwa alilipwa dola 100,000 kuficha video iliyokuwa inamuonesha Diddy akimpiga aliyekuwa mpenzi wake Cassie Ventura.
Jumanne, Juni 3,2025 Garcia alitoa ushahidi huo mahakamani akisema Sean "Diddy" Combs alimlipa dola 100,000 ndani ya mfuko wa karatasi wa rangi ya kahawia ili kupata video ya usalama iliyomnasa akimpiga mpenzi wake wa muda mrefu, Cassie katika hoteli moja jijini Los Angeles mwaka 2016.
Garcia alieleza kuwa Machi 5, 2016, baada ya tukio hilo katika hoteli ya InterContinental, alipokea simu kutoka kwa mfanyakazi wa Combs, Kristina Khorram, aliyemuuliza kama kuna uwezekano wa kupata au kuangalia nakala ya video hiyo ambapo Garcia alijibu hapana kisha akakata simu.
Aliendelea kueleza kuwa jioni hiyo alipokea simu nyingine kutoka kwa Khorram, ambaye aliwaunganisha moja kwa moja na Diddy. Garcia alisema msanii huyo alionekana mwenye wasiwasi kwenye simu na alikiri kuwa alikunywa sana siku hiyo ya tukio na kwamba video hiyo ingesambazwa mitandaoni ingeweza kumuharibia kazi yake.
Garcia aliiambia mahakama kuwa alimjibu Diddy kuwa hatoweza kumsaidia kwa sababu hawezi kufikia chumba ambacho kinahifadhiwa seva ya video lakini Khorram na Diddy walimpigia tena na Diddy akamuomba amjali hata kwa mara moja jambo ambalo lilimfanya msaidizi huyo kumsaidia Diddy.
Alikwenda kuzungumza na msimamizi wake ambaye alikubali kuuza video hiyo kwa dola 50,000. Msimamizi huyo alimpa USB yenye nakala ya video na siku iliyofuata, Garcia aliifikisha kwenye anwani moja huko Los Angeles, ambako alikutana na Diddy, Khorram, na mlinzi.
Aidha alikabidhi USB hiyo kwa Diddy kisha msanii huyo alimpigia Ventura kupitia FaceTime akampa simu Garcia azungumze naye ambapo Cassie alimwambia mlinzi huyo kuwa alikuwa na filamu inayotarajiwa hivyo si wakati mzuri wa video hiyo kuvuja.
Mlizi huyo ambaye alikuwa akilipwa dola 10.50 kwa saa, alisaini nyaraka zilizooneshwa kwa majaji zikisema amekabidhi nakala pekee ya video hiyo pamoja na kusaini mkataba wa kutotoa siri (nondisclosure agreement) uliokuwa na adhabu ya dola milioni moja endapo angekiuka makubaliano hayo.
Baada ya kusaini, Combs alitoka nje ya chumba kisha akarudi na mfuko wa karatasi na mashine ya kuhesabia fedha. Alianza kuweka mafungu ya dola 10,000 kwenye mashine hadi ilipoonyesha jumla ya dola 100,000 mara mbili ya kiasi kilichoombwa na msimamizi wake.
Garcia alisema alielewa kuwa nyongeza ya dola 50,000 ilikuwa kwa ajili yake na mfanyakazi mwenzake huku Diddy akimsihi asiende kununua vitu ambavyo vitatumia gharama kubwa ambapo mlinzi huyo alieleza kuwa alitumia dola 30,000 kununua gari used.
Mbali na huyo shahidi mwingine alipanda kizimbani ambaye alikuwa Afisa Mkuu wa Fedha wa lebo ya Bad Boy Records, Derek Ferguson akikiri kuwa Diddy alitumia kadi moja ya mkopo kwa matumizi binafsi na biashara, jambo linaloonyesha uwezekano wa matumizi mabaya ya fedha.
Diddy anakabiliwa na mashtaka ya usafirishaji wa binadamu kwa ajili ya ngono, njama ya kihalifu (racketeering), na usafirishaji kwa lengo la kushiriki katika ukahaba. Amekana mashitaka yote na endapo atapatikana na hatia, anaweza kuhukumiwa kifungo cha maisha gerezani.
Leave a Reply