Mwanamuziki wa Singeli, Mussa Ramadhan maarufu ‘Dj Mushizo’ amefikisha wiki ya pili akiwa hospitali kutokana na ajali ya moto aliyopata nyumbani kwake.
Akizungumza na Mwananchi, meneja wa Mushizo, Ally Masupu ameeleza hali ya msanii huyo huku akiweka wazi kinachochelewesha kuruhusiwa kutoka hospitali.
“Bado anaumwa yupo Hospitali ya Amana anapatiwa matibabu, hajapewa ruhusa kwa sababu majeraha ya moto (vidonda) hayajakauka vizuri.
"Sehemu ambazo bado zina shida kidogo pia zimeathirika kwa kiasi kikubwa ni mikononi, mgongoni pamoja na kwenye shingo, kuhusu kuruhusiwa labda kwa wiki ijayo lakini kwasasa bado yupo Amana anaendelea na matibabu,” amesema Masupu.
Aidha ameongezea kwa kueleza: “Hali yake anaendelea vizuri baadhi ya vitu vyake anafanya mwenyewe hata simu anatumia lakini sasa hivi nipo nayo mimi kwa sababu wamemuingiza kumsafisha vidonda.”
Ikumbukwe msanii huyo alipata ajali ya moto nyumbani kwake Tabata jijini Dar es Salaam majira ya 12 jioni, Juni 12, 2025 huku chanzo cha moto kikitajwa kuwa ni shoti ya umeme.
Nyimbo zilizompa umaarufu Mushizo ni Wivu pamoja na Mapenzi Hisia, ambazo zinafanya vizuri kwa sasa.

Leave a Reply