Hatma ya Diddy kujulikana hivi karibuni

Hatma ya Diddy kujulikana hivi karibuni


Mahakama ya jijini Manhattan imeendelea na kesi ya Sean “Diddy” Combs ambapo kwa sasa inaelezwa kesi hiyo ipo ukingoni huku hatma ya rapa huyo kujulikana hivi karibuni.

Juni 23,2025 upande wa mashtaka ulipeleka shahidi wa 34 na wa mwisho ambaye ni Afisa Maalum wa Usalama wa Ndani Joseph Cerciello, ambaye ushuhuda wake uliangazia siku 28 kutoka mwanzo wa kesi mpaka sasa.

Katika ushahidi wake Afisa Cerciello alieleza kuwa uchunguzi ulionesha mifumo yote ambayo Diddy alikuwa akiitumia kusafirisha wanawake kwa ajili ya biashara za kingono akitumia ushawishi wake katika muziki ili kudhibiti wanawake hao.

Aidha Cerciello alionesha rekodi za safari, mawasiliano ya kidigitali, video na mashahidi waliolazimisha kushiriki kwenye matukio ya kingono.

Katika siku hiyo hiyo tukio jingine ambalo liliwashangaza wengi ni baada ya mawakili wa Diddy akiongozwa na Marc Agnifilo kutangaza kutokuwa na mpango wa kupeleka mashahidi kwa ajili ya kumtetea rapa huyo.

Utakumbuka wiki iliyopita mawakili hao walipanga kupeleka mashahidi watatu akiwemo Diddy mwenyewe, msaidizi wa Combs Enterprises pamoja na mtaalamu wa saikolojia. Hata hivyo kwa mujibu wa mwanasheria mstaafu Mark Chutkow ameeleza kuwa uamuzi huo ni wa busara kwani utaepusha maswali yatakayo mchanganya Diddy.

Hata hivyo baada ya ushahidi kukamilika Juni 26 viongozi wa pande zote watatoa hoja zao za mwisho, kisha wajumbe wa mahakama ya kisheria wataanza mjadala wa mwisho na uamuzi wa hatima ya kesi hiyo. Kwa sasa, Diddy amekana mashtaka yote huku akikataliwa dhamana mara tatu kutokana na hofu ya kuwahonga mashahidi.

Baadhi ya mashahidi wa muhimu waliotoa ushahidi wa kuathiriwa na matukio ya kingono ni pamoja na wapenzi wa zamani wa Diddy, Jane na Cassie huku wengine ni pamoja na rapa Kid Cudi, mlinzi wa nyumbani kwa Diddy, Mia, Capricorn Clark, Kerry Morgan, Bryana Bongolan na wengineo.

Diddy anakabiliwa na mashtaka ya usafirishaji wa binadamu kwa ajili ya ngono, njama ya kihalifu (racketeering) na usafirishaji kwa lengo la kushiriki katika ukahaba. Licha ya kukana mashtaka yote. Endapo rapa huyo atapatikana na hatia anaweza kuhukumiwa kifungo cha maisha gerezani.

Sean "Diddy" Combs alikamatwa Septemba 16, 2024 katika hoteli ya Park Hyatt, Manhattan, New York na kupelekwa moja kwa moja katika gereza la Metropolitan huko Brooklyn. Kesi yake ilianza kusikilizwa Mei 5,2025.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post

Latest Tags