Ndumbaro: Filamu zitumike kukuza ushirikiano baina ya Tanzania na China

Ndumbaro: Filamu zitumike kukuza ushirikiano baina ya Tanzania na China

Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo Damas Ndumbaro wakati akitoa hotuba katika uzinduzi wa filamu ya Kichina iliyotafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili amesema ushirikiano wa kidiplomasia baina ya Tanzania na China wenye miaka 56 sasa, unazidi kuendelezwa kupitia shughuli mbalimbali za kiuchumi, biashara, miundombinu, kilimo, matibabu,filamu na jamii.

Filamu hiyo iliyopewa jina “Welcome to Milele” imechezwa na wasanii kutoka China na Tanzania ikiwa na lengo la kudumisha ushirikiano baina ya Tanzania na China tangu kuanzishwa kwake mwaka 1968.
Uzinduzi huo umefanyika katika hafla fupi ndani ya viunga vya Azam Tv jijini Dar es Salaam, huku ukiwa umehudhuriwa na wanafunzi na wageni mbalimbali akiwemo balozi wa China nchini Tanzania Chen Mingjian.

Ndumbaro amesema, baada ya miongo sita ya ushirikiano wa dhati na urafiki kati ya nchi hizi mbili kumezaa matunda kwenye uchumi, biashara, miundombinu, kilimo, matibabu, afya na umepata matokeo ya kuvutia.

"Hadi sasa, madaktari wa China wametibu zaidi ya watu milioni 3.6 wa Tanzania na wakati huohuo kuchangia uboreshaji wa mazingira ya huduma mbalimbali hapa nchini,” amesema.

Ameeleza, uhusiano huo wa kitamaduni katika filamu hiyo umeashiria ubadilishanaji mzuri wa sanaa, fasihi,elimu na kudumisha utayarishaji na usambazaji wa filamu hiyo lakini pia uanzishwaji wa Taasisi ya Confucius Tanzania itayorahisisha ufundishaji wa lugha na tamaduni za Kichina hapa nchini.

Aidha, kwa upande wake balozi wa China nchini Tanzania Chen Mingjian ametoa shukrani zake za dhati kwa serikali ya Tanzania kwa kutoa ushirikiano na kufanikisha utengenezwaji wa filamu hiyo iliyoanza kuruka rasmi Agosti 5,2024 ndani ya kituo cha Azam Tv huku ikitarajiwa kuisha Septemba 29, 2024.

Awali mwaka 2022, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan na Rais wa China Xi Jinping walitangaza kuboresha ushirikiano wa kina ili kukuza na kuendeleza ushirikiano wa pande zote mbili na kuamua kuadhimisha miaka 56 ya uhusiano huo Wakidiplomasia.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Christina Lucas


Latest Post