Kiu ya mashabiki wengi wa Bongofleva kwa sasa ni kuona Mbosso anakuja vipi na kazi yake ya kwanza baada ya kuachana na WCB Wasafi, rekodi lebo yake Diamond Platnumz ambayo kafanya nayo kazi kwa miaka saba.
Huu ndio mtihani unaomkali Mbosso wakati huu na pengine ndio utatoa picha kamili ya safari yake nje ya lebo itakavyokuwa, hii ni karata muhimu kwake naye anajua hilo na ndio sababu anaonekana kujipanga vizuri.
Utakumbuka kuwa Mbosso aliyetamba na kibao chake, Hodari (2018), ni msanii wa sita kutambulishwa na WCB Wasafi baada ya Harmonize (2015), Rayvanny (2016), Queen Darleen (2016), Rich Mavoko (2016) na Lala Lava (2017).
Mbosso aliyeanza safari ya muziki Poteza Records chini ya Sule, alitambulishwa WCB Wasafi hapo Januari 2018 baada ya kuachana na kundi la Yamoto Band ambalo alikuwa na wenzake watatu, Enock Bella, Beka Flavour na Aslay.
Wimbo wake mwisho kuachia chini ya lebo hiyo unaitwa 'Kupenda' uliotayarishwa na Laizer Classic wa Wasafi Records, huu ulitoka Januari 10, 2025 na tayari huko YouTube umetazamwa zaidi ya mara milioni 5.9.
Kupitia mitandao ya kijamii tayari Mbosso ameanza kudokeza ujio wake mpya, anaweza kuja na wimbo, EP au albamu ambayo itakuwa ya pili katika safari yake ya muziki baada ya hapo awali kutoa, Definition of Love (2021) yenye nyimbo 12.
Ikiwa Mbosso atakuja na wimbo, basi mashabiki wataanza kulinganisha na zile alizotoa chini ya WCB Wasafi na kubwa zaidi ni namba utakazopata katika majukwaa ya kidijitali ya kusikiliza muziki.
Ikumbukwe Harmonize alipoachana na WCB Wasafi wimbo wake kwanza kutoa ni Uno (2019), Rich Mavoko kazi yake kwanza ilikuwa ni Ndegele (2018), naye Rayvanny akaanza na Pele Pele (2022) akimshirikisha Luana Vjollca kutokea Albania.
Licha ya kazi hizo kufanya vizuri na pamoja na nyingine walizokuja kutoa hapo baadaye, bado Harmonize, Rich Mavoko anahukumiwa kwa kushindwa kutengeneza nyimbo zilizopata namba kubwa kuzidi zile walizotoa wakiwa Wasafi.
Mathalani Harmonize, video ya wimbo 'Kwangwaru' iliyotoka Aprili 14, 2018 akimshirikisha Diamond Platnumz, ndio iliyofanya vizuri zaidi YouTube upande wake ikiwa imetazamwa zaidi ya mara milioni 127.
Baada ya Kwagwaru video za nyimbo zake zilizofanya vizuri ni Happy Birthday (2017) - milioni 55, kisha inafuatia Bado (2016)- milioni 55, ambao pia alimshirikisha Diamond, kazi zote hizi zilitoka chini ya WCB Wasafi.
Ikiwa ni zaidi ya miaka mitano tangu kuondoka katika lebo hiyo hakuna wimbo aliotoa ukafikia hizo, ngoma yake, Single Again (2023) ndio unapanda polepole ambapo video yake hadi sasa imetazamwa zaidi ya mara milioni 38.
Na huu ndio mtihani wa kwanza atakaokumbana nao Mbosso nje ya WCB Wasafi, na sio yeye tu, bali wasanii wote wanaoachana na lebo za hawa wasanii maarufu wamekuwa wakuhukumiwa sana kwa kutumia kigezo hiki.
Hadi sasa Mbosso wimbo wake uliofanya vizuri zaidi YouTube ni Baikoko (2021) akiwa na Diamond, hivyo baadhi ya mashabiki ili waamini amefanikiwa kufanya vizuri nje ya Wasafi, basi atoe kazi itakayokuwa na namba za juu kuliko Baikoko.
Mbali na hayo, pia mashabiki wanataka kuona kama ataendelea kufanya kazi na Diamond ambaye kazi zao zilifanya vizuri wakitoa kolabo tano pamoja ambazo ni Jibebe (2018), Baikoko (2021), Karibu (2021), Oka (2022) na Yataniua (2022).
Huyu ni msanii wa kwanza wa WCB Wasafi kutoa albamu na kumshirikisha Diamond kwenye nyimbo mbili kwa wakati mmoja, kisha akafuata D Voice kupitia albamu yake, Swahili Kid (2023) iliyomtambulisha.
Utakumbuka Mbosso ndiye msanii pekee wa Wasafi aliyefanikiwa kufanya nyimbo mbili na wazazi wenza wa Diamond ambao ni Hamisa Mobetto na Tanasha Donna, nyimbo walizotoa pamoja ni 'Jibebe' na 'La Vie' kutoka katika EP ya Tanasha, Donnatella (2020).
Hadi anaondoka WCB Wasafi, Mbosso alikuwa ametoa albamu moja, Definition of Love (2021), EP moja, Khan (2022), ameshinda tuzo moja ya muziki Tanzania (TMA) Msanii Bora wa Kiume wa Bongofleva 2022, huku akishirikiana na wasanii wengi wa kimataifa.
Baadhi ya wasanii wa kimataifa aliofanya nao kazi ni Mr. Flavour, Reekado Banks na Liya (Nigeria), Costa Titch na Chley (Afrika Kusini), Bahati (Kenya), Spice Diana (Uganda) na Innoss'B (DR Congo) ambaye pia kashirikiana na Diamond, Rayvanny na Zuchu.
Leave a Reply