Lebo hiyo imeeleza kuwa inafahamu madai yote yanayosambazwa katika mitandao mbalimbali ya kijamii na vyomba vya habari lakini hawawezi kuongelea masuala yoyote yanayohusu kazi zao kupitia mitandao ya kijamii au mifumo isiyo rasmi.
Bxtra wamesema kuwa wao ni kampuni inayosimamiwa kitaalamu na kufanya kazi kwa weledi na uwazi, pia wamesema wanaheshimu haki ya kila mtu kujieleza na kutoa taarifa.

Taarifa hiyo ya Bxtra inakuja kufuatia msanii chipukizi wa muziki wa Bongo Fleva, Cherry ambaye kupitia mitandao ya kijamii alidai kupitia magumu akiwa katika lebo hiyo ikiwemo manyanyaso ya kimkataba na unyanyasaji wa kingono.
Kupitia ujumbe uliochapishwa kwenye ukurasa wake wa Instagram, Cherry anadai kuwa alisaini mkataba wa miaka saba na lebo hiyo lakini ndani ya miaka mitatu amefanikiwa kuachia nyimbo mbili tu, video moja na EP moja iliyodhaminiwa na DSTV.
Licha ya mafanikio hayo ya awali anadai hajawahi kulipwa posho, kodi wala kupata marupurupu yoyote kutoka kwenye lebo hiyo.
Hata hivyo ameweka wazi kuwa alipotoa wazo la kujiondoa kwenye lebo hiyo ili ajitegemee na kuendelea na maisha yake ya muziki, aliambiwa alipe kiasi cha shilingi milioni 109 kama fidia kwa nyimbo 22 alizorekodi chini ya lebo.
Zaidi ya hayo, anasema kila anapojaribu kutoa muziki wake binafsi kwa gharama zake mwenyewe, lebo hiyo hufanya mawasiliano na wasambazaji wa muziki na kuzuia nyimbo zake kuwekwa kwenye majukwaa ya kidigitali.
“Sina uhuru wowote kama msanii. Hii miaka minne iliyobaki kwenye mkataba ni kama kifungo. Nina ushahidi na majina ya wahusika wa rushwa za ngono na unyanyasaji wa kijinsia katika tasnia, nitayaweka wazi. Lakini kwa sasa, nahitaji msaada kutoka kwa wanahabari na Baraza la Sanaa Tanzania @basata.tanzania ”
Leave a Reply