Ustaa Unavyomtesa Chris Brown

Ustaa Unavyomtesa Chris Brown

Mwanamuziki kutoka Marekani, Chris Brown ‘Breezy’ ameweka wazi kuwa maisha ya umaarufu yamekuwa na athari kubwa katika afya yake ya akili, huku akieleza kuwa kuna nyakati hutoroka usiku na kwenda kutembea mitaani ili ajisikie kama binadamu wa kawaida.

Kwenye moja ya mahojiano yake Breezy ameeleza kuwa licha ya mafanikio makubwa aliyonayo kuna wakati anahisi kupoteza uhuru wake wa kuishi maisha ya kawaida, na jambo ambalo analifanya ili aweze kupata furaha hata kwa mara moja ni kubadilisha mwonekano wake kwa kuvaa kofia kubwa, miwani au kujifunika sura ili apite mtaani pasipo watu kumtambua.

Ameeleza kuwa kwa kufanya hivyo, kunampa muda wa kubadilisha mazingira, kufikiria, au hata kula chakula kwenye mgahawa wa kawaida kama mtu wa kawaida, bila presha wala kamera za paparazi.

Mbali na hayo ameeleza kuwa kufanya hivyo sio kuficha uhalisia wake bali kujirudisha kwenye hali ya kibinadamu kwani maisha ya umaarufu yanaweza kumfanya msanii ajisikie kama bidhaa, na kusahau kuwa yeye ni binadamu anayehitaji uhuru, utulivu na maisha ya kawaida. Aliongeza kuwa kutoroka usiku humfanya ajikumbushe kuwa bado ana maisha nje ya jukwaa, kamera, na mitandao ya kijamii.

Kufuatia na mtiririko huo mpya wa maisha, Brown amewataka wasanii wengine kuutendea haki upande wao wa pili wa maisha nje ya ustaa, kwani anaamini bado kuna mengi mazuri na yenye thamani katika kuwa "Chris" na si "Chris Brown" anayetambulika duniani kote.

Chris Brown alianza muziki rasmi mwaka 2005, akiwa na umri wa miaka 16, alipoachia albamu yake ya kwanza "Chris Brown" ambayo ilijumuisha hiti kubwa kama "Run It!" iliyomfanya apate mafanikio ya haraka duniani, ametamba na ngoma mbalimbali zikiwemo Sensational, Shooter, Press Me, Night Off na nyinginezo.

Aidha mbali na yeye kutoa ushauri huo kwa mastaa wengine naye mwanamuziki wa Hip Hop kutoka Bongo, Billnass mapema leo alitoa ushauri kwa wasanii chipukizi akiwataka kuwa wastahamilivu kwani tasnia imejaa mambo mengi mabaya nje ya umaarufu.

“To all Young People, Wadogo zangu na rafiki zangu miliobarikiwa vipaji mbalimbali, Kabla ya kuingia kwenye tasnia yoyote inayohusiana na umaarufu Tanzania!! Muombe sana Mungu akupe nguvu ya uvumilivu na Roho ya kustahimili!! huku kuna kila aina ya vita, Usaliti, Ushetani, Dhuruma kuanzia kwa wadau, Managers, Distribution Company, Labels n.k.

Swala la kutajilika au kupata pesa kupitia hizi kazi sio rahisi kama unavosikia ila kupata msongo wa mawazo, kupoteza maisha, kupata maradhi, kuchanganyikiwa ama kuingia kwenye Addiction mbalimbali ni rahisi kuliko kutengeneza pesa, ni vyema kuwa na umakini sana na kuingia kwenye tasnia ukiwa na utayari lakini usiache kumuweka Mungu kwanza,”ameandika Nenga

Aidha ameongezea kwa kuandika “Maana unaweza kupambana ili uisaidie familia yako kumbe unaenda kuleta janga ambalo familia yako ndio itakuwa kwenye jukumu la kuteseka kukusaidia," Ameandika.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post

Latest Tags