Jina la Taylor Terry huenda si maarufu kwa watu wasiopendelea mitandao ya kijamii, lakini katika ulimwengu wa TikTok mwanadada huyo amekuwa akifuatiliwa zaidi kupitia video zake zikimuonesha akidansi pembeni ya mkali wa R&B, Chris Brown.
Wakati wa show, macho ya wengi huwa kwa Chris Brown, lakini nyuma yake ipo timu ya dansi ambayo inahakikisha onesho linakuwa la kipekee na Taylor ni mmoja wao, ambaye amekuwa akifuatiliwa zaidi katika mitandao ya kijamii.
Taylor amekuwa akiwavuruga wengi hasa kufuatia utashi wake katika kudansi pamoja na ujasiri anaouonesha jukwaani jambo ambalo limekuwa likizua shangwe kwa mashabiki wakati wa show.
Safari yake ya dansi ilianza tangu akiwa mtoto, akihudhuria madarasa ya dansi karibu na nyumbani kwao huko Texas, Marekani ambapo alianza kujifunza mitindo mbalimbali ikiwemo ya hip-hop, jazz, na contemporary, huku miaka michache baadaye akahamia Los Angeles kwa ajili ya kupambania ndoto zake.
Mwaka 2021, ndoto yake ilitimia alipochaguliwa kujiunga na timu ya dansi ya Chris Brown. Tangu wakati huo, ameshiriki katika video mbalimbali kama “Under the Influence”, “WE (Warm Embrace)”, na maonesho ya moja kwa moja duniani kote ikiwemo Afrika.
Uwepo wa Taylor katika maonesho ya Brown barani Afrika, umevutia mashabiki wengi, tangu alivyoonesha uwezo wake katika ziara ya “Under the Influence Tour”, ambapo mashabiki wamekuwa wakimfuatilia hasa katika mtandao wa TikTok wakimpongeza kwa uwezo mkubwa kwenye dansi na ushirikiano mzuri kwa Breezy.
Nje ya dansi, Taylor ni mtayarishaji wa maudhui ya mitandao ya kijamii, mwanamitindo na mtoa mafunzo ya dansi. Ambapo amekuwa akitumia akaunti zake za mitandao ya kijamii kuwahamasisha wasichana wenye ngozi nyeusi ambao wanatamani kufika mbali kwenye sanaa.
“Najua kuwa si rahisi kwa msichana mweusi kupenya katika sekta hii, lakini ninaamini katika kazi, nidhamu na kuwa halisi,” amezungumza kwenye moja ya mahojiano yake.
Kwa mujibu wa vyanzo vya karibu vya mwanadada huyo, vinaeleza nje ya kudansi kwenye majukwaa makubwa na Breezy, yeye ni mke wa mtu ameolewa na mume wake anajivunia kwa kazi anayoifanya, lakini mwanadada huyo hajathibitisha kuolewa kwake.

Leave a Reply