Kampuni ya Recording Academy ambao ni wagawaji wa tuzo za Grammys wametangaza mabadiliko katika tuzo hizo kwa mwaka 2026 ambapo watagawanya tuzo ya ‘Best Country Album’ kuwa katika vipengele viwili vipya Best Contemporary Country Album na Best Traditional Country Album.
Uamuzi huu unakuja baada ya ushindi mkubwa wa albamu ya Beyoncé ‘Cowboy Carter’, ambayo ilishinda tuzo ya Best Country Album kwenye Grammys za mwaka 2025.
Mkurugenzi Mtendaji wa Recording Academy, Harvey Mason Jr., aliambia Billboard kuwa tasnia ya muziki wa country inahitaji nafasi zaidi ili muziki kuheshimiwa zaidi.
“Jumuiya ya muziki wa country ilisema, tunaamini tunahitaji nafasi zaidi ili muziki wetu uweze kusherehekewa na kuheshimiwa. Hii inafanya muziki wa country ulingane na kinachotokea kwenye aina nyingine za muziki, lakini pia inaunda nafasi kwa mwelekeo ambao aina hii ya muziki inaelekea.
Changamoto zimekuwa, kwa kawaida, kwamba watu wengi hawakuwa na uhakika kama [albamu fulani] ilikuwa Americana, roots, folk au country kwa hiyo walikuwa wanaweka kila kitu kwenye kipengele kimoja tu,”amesema Harvey Mason Jr
Aidha aliongezea kwa kueleza mabadiliko hayo yamefanywa kama ambavyo walifanya kwenye kipengele cha R&B kuwa Best R&B Performance na Best Traditional R&B Performance ili kuakisi maendeleo yanayoendelea ndani ya aina hiyo ya muziki kwa ujumla.
Tuzo hizo za 68th Grammy zinatalajiwa kutolewa Februari Mosi, 2026 katika ukumbi wa Crypto.com Arena, Los Angeles, Marekani ambapo nominees wataanza kutangazwa Novemba 7,2025.
Wasanii na watayarishaji watawasilisha kazi zao ndani ya OEP kuanzia 16 Julai hadi 29 Agosti 2025, huku watu wakianza kupiga kura 2 Desemba 2025 hadi 5 Januari 2026.

Leave a Reply