Safari mpya ya Mbosso, mastaa wampa maua yake

Safari mpya ya Mbosso, mastaa wampa maua yake

Wakati wakazi wa jiji la Dar es Salaam wakiwa wametulia usiku majumbani kwao wakitumia muda huo kupumzika, kwa upande wa mwanamuziki Mbosso usiku wa kuamkia leo Juni 13,2025 ulikuwa wa tofauti kwani alianza safari yake mpya ya kimuziki tangu kuachana na lebo ya Wasafi na kutoa Ep yenye nyimbo saba.

Utakumbuka taarifa za Mbosso kuondoka katika lebo ya WCB zilianza mapema mwaka huu, huku uvumi huo ukithibitishwa na Mkurugenzi wa lebo hiyo, Diamond Platnumz Februari, 2025.

Akiwa msanii huru Mbosso ameachia Ep inayotambulika kwa jina la ‘Room Number 3’ iliyobeba ngoma Saba ikiwemo Pawa, Nusu Saa, Tena, Merijaah. Siko Single, Aviola, Asumani lakini pia kuna Bonus Track.

Wakati akizungumza kwenye uzinduzi huo Mbosso ameeleza maana ya jina la Ep yake huku ikigusia maisha yake alipokuwa Mkubwa na Wanaye pamoja na WCB.

“Jamani ‘Room Number 3’ sio Lodge niwaambie mapema sio guest house, ni safari ya ukuaji ya maisha ya kimuziki ya Mbosso ambaye ni Mbwana Yusuph Kirungi, Room Number 1 ambayo haionekani maanaa yake tuliimaliza kwa muda mrefu, hichi ni chumba ambacho ninakishukuru sana kwenye maisha yangu ya kimuziki kwa sababu kilinitambulisha kwa watu wote ambao walikuwa hawamfahamu Mbosso.

Shukrani nyingi kwa Mkubwa Fella, lakini pia shukrani nyingi kwa Aslay, kwanini nasema Aslay kipindi naanza muziki siku yangu ya kwanza mimi kuwa msanii wa Mkubwa na Wanae ni kwasababu nilimuona Aslay anaimba na nikamsikia Mkubwa Fella anahitaji vijana wenye rika kama lake. Kwahiyo kupitia Aslay nikapata confidence ya kuwa namimi ninaweza kuimba,”amesema Mbosso

Aidha ameendelea kwa kueleza maana ya jina hilo kwa kusema
“Room Number 2 ilikuwa ni maisha mazuri sana ya muziki wangu yenye upendo, furaha, marafiki ambao tulikuwa tumeshibana vijana wenzangu wote tuliokuwa tunaiunganisha Wasafi, Kiongozi wetu Daimond, Harmonize, Rayvanny, Lavalava, Queen Darleen, Rich Mavoko mpaka tumekuja kumpata Zuchu, pamoja na D Voice hayo yalikuwa maisha mazuri sana.

Niliona utamu na sukari ya muziki wangu, nilionana na matajiri kupitia Wasafi, watu wenye thamani, shukrani kwa Diamond hata hii kujiamini kusimama hapa mbele nimejifunza kutoka kwake,”amesema Mbosso

Hata hivyo aliendelea kwa kueleza maana ya Room Number 3 ambapo aliweka wazi kuwa ndio safari yake mpya anayoianza sasa akiwa ameachia Ep hiyo tangu kutemana na WCB.

Mastaa wampa maua yake

Mocco
“Mimi nafurahi kuona jitihada zake, kazi zinaenda zinafanya vizuri, nadhani ni miongoni mwa msanii ambaye tunzi zake zinapendwa na kila mtu wewe ukitaka kuona Mbosso ni msanii Fulani noma harafu watu hawampi heshima yake wewe posti picha na mtu yoyote harafu sema mkali ni nani, wewe utaona tuu reaction za watu kwahiyo mimi namkubali sana. ukiachana urafiki wetu mimi ni shabiki yake mkubwa,”

Yammi
“Mbosso ni msanii mzuri, anasauti, anaimba vizuri, mimi ni shabiki wake tangu mwanzao, anaandika mashairi mazuri kwahiyo navutiwa na yeye na vitu vingi kwenye kazi, anaandika mashairi yanayopendeza masikioni mwa watu. Namuombea tuu kwa Mungu amuongoze kwenye kila jambo analolitaka liweze kuwa,”

Young Lunya
“Nakumbuka kipindi anakuja Mkubwa na Wanae aliimba wimbo huo na kila mtu alimkubali, mimi nilikuwa ni mmoja wa watu ambao nilimkubali sana yeye mwenyewe pia alikuwa ananipenda, alikuwa anapenda sana kuniandikia Chorus, kwahiyo ni msanii mzuri namjua zaidi ya miaka kumi najua uwezo wake. Nyimbo zote nikali sana kwahiyo endelea kutengeneza muziki mzuri na Mungu akubariki sana,”amesema

Hata hivyo kwa upande wa Diamond ambaye alikuwa bosi wake amempongeza msanii huyo kwa akishare kava ya Ep na kuweka wazi kuukubali wimbo wa ‘Pawa’ ambao aliutuma uwe special kwa mke wake Zuchu.

Kauli ya BASATA

Aidha Baraza la Sanaa Taifa ‘Basata’ chini ya Katibu mtendani wa baraza hilo Kedmon Mapana amempongeza msanii huyo kwa hatua hiyo kubwa.

“Mbosso tunakupongeza sana sisi kama Baraza la Sanaa Taifa na hiyo Room Number 3 uliyosema sisi kama Basata tulikuwa wa kwanza kuisikiliza yani katika nyimbo zote saba hakuna hata mmoja tuliosema isubiri kidogo.

Siyo Ep yake tuu lakini kuna mambo mengine mzuri ametushirikisha kwamba pia atatambulisha Bendi, lakini ataenda mbali zaidi atakuwa msanii wa kwanza ambaye atakwenda kumiliki majukwaa na sound system kubwa. Kwahiyo anakwambia ukitaka kumchukua yeye atakuja na package yote, na sisi kama Basata tunajivunia kwa wasanii wetu wanazidi kukua na pale wanapokwenda kujitegemea,”amesema Mapana

Hii ni kazi ya kwanza kwa msanii huyo kuachia tangu kutemana na Wasafi. Hata hivyo hivi karibuni msanii hyo alishirikishwa kwenye kazi za wasanii wengine kama 'Boda' ya Billnass na 'Look for Love' ya Darassa.

Wimbo wake wa mwisho kuachia chini ya lebo hiyo unaitwa 'Kupenda' uliotayarishwa na Laizer Classic, ambao ulitoka Januari 10, 2025 na tayari huko YouTube umetazamwa zaidi ya mara milioni 5.9

Hadi anaondoka WCB Wasafi, Mbosso alikuwa ametoa albamu moja, Definition of Love (2021), EP moja, Khan (2022) ambapo Room Number 3 (2025) itakuwa Ep yake ya pili.

Mbali na kutoa ngoma hizo, lakini pia Mbosso amefanya kolabo na wasanii wa kimataifa akiwemo Mr. Flavour, Reekado Banks na Liya (Nigeria), Costa Titch na Chley (Afrika Kusini), Bahati (Kenya), Spice Diana (Uganda) na Innoss'B (DR Congo) ambaye pia kashirikiana na Diamond, Rayvanny na Zuchu.

Katika muda aliokuwa ndani ya WCB kuanzia Januari 2018 hadi Februari 2025, Mbosso amewahi kushinda tuzo moja ya muziki Tanzania (TMA) kama Msanii Bora wa Kiume wa Bongofleva 2022.riptions






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post

Latest Tags