Taylor Swift, Post Malone wafunika tuzo za MTV VMAS 2024

Taylor Swift, Post Malone wafunika tuzo za MTV VMAS 2024

Katika Tuzo za MTV VMAs 2024 zilizotolewa jana Septemba 12 wanamuziki Taylor Swift na Post Malone waliibuka kidedea kwa kuondoka na tuzo nyingi zaidi huku‘kolabo’ yao ya ‘Fortnight’ ikiwabeba zaidi.

Wawili hao waliuteka usiku huo ambapo Taylor Swift aliteuliwa kuwania vipengele 12 alishinda saba huku kwa upande wa Post Malone aliteuliwa kuwania vipengele 11 na kuondoka na tuzo tano huku wimbo wao ukiondoka na tuzo ya Video Bora ya Mwaka.

Kupitia kipengele cha kwanza cha ‘Video of the Year’ waliokuwa wakiwania tuzo hiyo ni pamoja na Ariana Grande, Billie Eilish, Doja Cat, Eminem, SZA lakini tuzo hiyo waliondoka nayo Taylor Swift na Post Malone katika wimbo wa ‘Fortnight’.

Aidha katika kipengele cha ‘Artist of the Year’ tuzo hiyo ilikwenda kwa Taylor Swift huku akiwapiku wenzake kama Ariana Grande, Bad Bunny, SZA, Sabrina Carpenter, Eminem na Bad Bunny.

‘Song of the Year’ tuzo hiyo ilibebwa na nyota wa ngoma ya ‘Espresso’ Sabrina Carpenter ambapo amewapiga chini mastaa kama Beyoncé, Jack Harlow, Kendrick Lamar, Taylor Swift na Teddy Swims.

Upande wa ‘Best New Artist’ mwanamuziki Chappell Roan kupitia ngoma ya ‘Island’ amewashinda wenzake Gracie Abrams na Tyla, hata hivyo, katika kipengele cha ‘Best collaboration’ Taylor Swift na Post Malone waliibuka tena kidedea na kuwapiku mastaa kama GloRilla, Megan Thee Stallion, Drake Feat. Sexyy Red & SZA, Jessie Murph feat. Jelly Roll na Jung Kook feat. Latto.

Huku katika kipengele cha ‘Best Pop’ mwanadada Taylor Swift akanyakua tena tuzo hii iliyokuwa ikiwindwa na wasanii kama Camila Cabello, Dua Lipa, Olivia Rodrigo, Sabrina Carpenter na Tate McRae.

Mbali na hizo tuzo ambayo ilikuwa ikiwatoa macho wakali wa Hip hop Marekani ya ‘Best hip-hop’ iliondoka na Eminem akipiga chini mastaa wenzake akiwemo Travis Scott, Megan Thee Stallion, Drake, Gunna na GloRilla.

Aidha kwenye upande wa ‘Best R&B’ SZA amebeba tuzo hiyo iliyokuwa ikitolewa macho na wasanii Tyla, Victoria Monét, Usher, Muni Long na Alicia Keys. Hata hivyo kwenye kipengele cha ‘Best Afrobeats’ mrembo Tyla ameendelea kuwatoa jasho wasanii wenzake ambapo ameondoka na tuzo hiyo huku akiwapiku mastaa kama Ayra Starr, Burna Boy, Chris Brown, Tems na Usher.

Katika kipengele cha ‘Director of the Year’ ‘kolabo’ ya Taylor Swift na Post Malone ‘Fortnight’ imeibuka kwenye kinyang’anyiro hicho akiwapiku wanamuziki kama Eminem, Sabrina Carpenter, Ariana Grande, Megan Three Stallion na Bleachers.

‘Art Director of the Year’ mwanadada Megan Three Stallion aliondoka na tuzo katika kipengele hicho ambacho kilikuwa kinawashindanisha wasanii Taylor Swift, Post Malone, Charli XCX, Sabrina Carpenter, Olivia Rodrigo na Lisa.

Kwenye upande wa ‘Editing video of the year’ Taylor na Post Malone waliondoka na tuzo hiyo kupitia wimbo wa ‘Fortnight’ huku kipengele cha ‘Best Director’ mwanadada huyo aliondoka na tuzo hiyo ambapo imetokana na kuongoza mwenyewe kolabo hiyo.

Mbali na kuondoka na tuzo hizo mwanamuziki Taylor Swift amevunja rekodi ya Beyonce kwa kufikisha tuzo 30 huku Bey akiwa na tuzo 26 akifuatiwa na Eminem’s akiwa na tuzo 15 za MTV Video Music Awards.

Tuzo za Muziki za Video za MTV za 2024 zilifanyika UBS Arena huko Elmont, New York, usiku wa kuamkia leo Septemba 12, 2024.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post