Rapa maarufu na mwenye ushawishi zaidi ulimwenguni kwasasa, Kendrick Lamar ameibuka kinara katika Tuzo za BET zilizofanyika usiku wa kuamkia leo Juni 10, 2025, hafla inayotambua na kuenzi wasanii, waigizaji na wanamichezo Weusi.
Mmiliki wa ngoma ya "30 For 30", Lamar ameshinda tuzo tano ambazo ni Msanii Bora wa Hip hop upande wa wanaume, Albamu Bora ya Mwaka, Video Bora ya Mwaka kupitia wimbo wake 'Not Like Us', Wimbo Bora wa Kushirikiana 'Luther' akiwa na mwanadada SZA, Lamar pia ameshinda tuzo ya muongozaji bora wa video wa mwaka na mshirika wake wa muda mrefu katika ubunifu 'Dave Free'. Utakumbuka kuwa rapa huyo pia aliibuka kinara kwenye tuzo za Grammy 2025 baada ya kushinda vingele vitano.
Lamar amesifia mchakato wa BET kuhakikisha wanathamini na kuenzi sanaa kwa watu weusi wakati anachukua tuzo ya Mtayarishaji Bora wa Video aliyoshinda pamoja na Dave Free katika hafla hiyo iliyofanyika ukumbi wa Peacock jijini Los Angeles na kurushwa moja kwa moja kupitia kituo cha televisheni cha BET.
“BET imekuwa ikihakikisha inawakilisha utamaduni kwa usahihi, na kila wakati imekuwa ikinipa nafasi kuwa sehemu ya kile tunachokiwakilisha,” alisema Lamar alipokuwa akipokea tuzo yake.
Mtangazaji wa hafla hiyo, mchekeshaji Kevin Hart, alifungua tukio hilo kwa kutambua maadhimisho ya miaka 25 ya Tuzo za BET na historia kubwa iliyowahi kuandikwa jukwaani hapo.
Hafla hiyo ilipitia historia ya muziki wa watu Weusi kwa kuanzia na onyesho kutoka kwa msanii wa R&B, Ashanti, aliyepiga mseto wa ngoma mbalimbali ikiwemo ile ya mwaka 2002 “Foolish.”
Maonyesho mengine ya burudani yalijumuisha midundo ya kisasa na ile miaka ya 2000 kama 'Ballin' kutoka kwa Mustard na Roddy Ricc, '1 Thing ' ya Amerie, na 'Like You' ya Bow Wow.
Hart aliongoza kwa ucheshi huku pia akiwatambua washindi wa tuzo ya heshima ya BET Ultimate Icon Award kwa mwaka huu, ambao ni Kirk Franklin, Mariah Carey, Jamie Foxx na Snoop Dogg.
Tuzo hiyo maalum ilitolewa kwa watu waliotoa mchango mkubwa katika muziki, burudani, utetezi wa haki na maendeleo ya jamii.
Ikiwasilishwa na gwiji Stevie Wonder, Jamie Foxx alipokea tuzo yake na kufunguka kuhusu safari yake ya kupona baada ya kupata kiharusi mwaka 2023.
“Lazima niseme ukweli, nilipoona kipande cha kumbukumbu ya waliotutoka (in memoriam), nilijisemea, ‘Hilo lingeweza kuwa la kwangu mimi’,” alisema Foxx kwa hisia.
Heshima nyingine ilimwendea rapa chipukizi Doechii ambaye alishinda tuzo ya Msanii Bora wa Hip hop upande wa wanawake. Utakumbuka pia msanii huyo aliibuka mshindi wa tuzo ya Albamu Bora ya Hip hop kupitia 'Alligator Bites Never Heal' kwenye tuzo za Grammy 2025.
Katika hotuba yake ya ushindi, Doechii aligusia maandamano dhidi ya ICE jijini Los Angeles, akisema, “Trump anatumia majeshi ya kijeshi kuwazuia waandamanaji.”
Aliongeza “Nataka mfikirie ni aina gani ya serikali hii, ambapo kila mara tunapotumia haki yetu ya kidemokrasia ya kuandamana, jeshi linatumwa kutukabili.”

Leave a Reply