Mwanamuziki wa Singeli nchini Msaga Sumu ameruhusiwa kutoka Taasisi ya Tiba na Mifupa, Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (MOI), baada ya kupata ajali ya gari wakati akirejea Dar es salaam akitokea Wilayani Namtumbo kutumbuiza kwenye mkesha wa Mwenge.
Akizungumza na Mwananchi Meneja wa msanii huyo Khalid Khalid 'Dj Msolopa' amesema kwa sasa Msaga Sumu anaendelea vizuri japo bado ana maumivu kwenye mbavu.
“Kwasasa yuko sawa na anaendelea vizuri ila anaendelea na mazoezi madogo madogo. Majibu ya daktari yanasema yako sawa na wamejiridhisha, wamemruhusu ila yupo tuu kwa ajili ya uangalizi.
"Hata simu bado hatujampa kwa sababu hatutaki aongee na watu. Ila yupo sawa anafanya mazoezi anatembea mwenyewe ila tumempa uangalizi wa kina kutokana na maumivu ya mbavu na bega lakini kichwani kote yuko sawa,”amesema
Aidha ameongezea kwa kusema “Ameruhusiwa yuko nyumbani ila tumempeleka kwa baba yake mkubwa Chanika. Hatujampeleka kwake moja kwa moja tumeogopa purukushani kwani anatakiwa akae kwanza sawa. Japo yupo sawa lakini tunataka akae sawa zaidi na baadaye akiwa vizuri tutamrudisha kwake,”amesema Meneja Msaga Sumu
Utakumbuka Msaga Sumu alipata ajali Mei 16,2025 wakati akirejea Dar es salaam akitokea Wilayani Namtumbo kutumbuiza kwenye mkesha wa Mwenge. Ameruhusiwa Mei 19,2025
Aidha awali akielezea chanzo cha ajali hiyo, meneja wake alisema chanzo cha ajali hiyo ni kukwepa bodaboda.
“Wakati tunarudi bodaboda alikatiza mbele yetu kwa hiyo dereva katika kumkwepa ndiyo kuna kitu akaparamia tukapinduka mara tatu. Kwa sasa hali yake sio mbaya yupo vizuri madaktari wanashughulika naye tunasubiri majibu ya moja kwa moja kutoka kwa daktari,” alisema.
Msaga Sugu amewahi kutamba na nyimbo kama vile Unanitega Shemeji, Cheupe Dawa, Kiki, Mambo Bado, Vikoba na nyinginezo akiwa anatajwa kama muasisi wa Muziki wa Singeli nchini.

Leave a Reply