Wanaochangia earphone hatarini kupata fangasi za masikio

Wanaochangia earphone hatarini kupata fangasi za masikio

Dar es Salaam. Kutokana na maendeleo ya teknolojia, kumekuwa na uzalishaji wa vitu vingi vyenye kurahisisha maisha ambavyo awali havikuwepo, huku wataalamu wa masuala hayo wakiendelea kubuni vitu vipya kila kukicha.

Hapo awali watu walisikiliza muziki kwa kutumia simu zao wakiwa wamezishika mkononi, huku sauti ya kinachosikilizwa ikisikika kwa kila mtu.

Kutokana na maendeleo ya teknolojia, kwa sasa ni nadra kukutana nalo kwani wengi hutumia vifaa mbalimbali vijulikanavyo kama spika za masikioni (earphone, head phone na ear pod) kwa ajili ya kuzuia sauti ya wanachosikiliza isisikike kwa watu wengine.

Katika matumizi ya vifaa hivyo kila mtu huwa na sababu zake, huku kukiwa na wale wanaodai kuwa hulazimika kutumia kwa ajili ya kutosumbua wengine.

Licha ya mazuri hayo yote, jambo lililozoeleka miongoni mwa watu hasa wanaokaa pamoja muda mwingi ikiwemo vyuoni, maofisini na katika shughuli mbalimbali ni kuazimana hivi vifaa vya masikioni.

Mkuu wa Kitengo cha Masikio, Pua na Koo, Dk Bukanu Faustine kutoka hospital ya Benjamin Mkapa, jijini Dodoma amesema wengi huazimana bila kujali afya za masikio ya yule anaye muazima, hali ambayo humfanya kuyaweka rehani masikio yake.

"Kwa watu wanaopenda kuazimana vifaa hivyo, wapo kwenye hatari kubwa ya kuambukizana ugonjwa wa fangasi kwenye masikio," amesema Dk Banaku.

Hata hivyo Mkurugenzi wa upasuaji wa masikio, pua na koo kutoka hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila ametaja sababu ya maambukizi ya fangasi za masikio pia hutokea wakati wa kuogolea.
"fangasi za masikio pia mtu anaweza kuambukizwa wakati wa kuogelea, maji yakiingia masikioni kwa mwenye fangasi hizi, mwingine akija anaweza kupata maambukizi," amesema Dk Mfuko.

Watumiaji
Mmoja kati ya watumiaji wa vifaa hivyo kutoka Kigogo, jijini Dar es Salaam ambaye hajataka jina lake liandikwe, anasema anapenda kuvaa earphone kwa sababu humsadia kusikiliza ujumbe kwa makini bila kelele yoyote.

Lakini pia anaeleze hutumia vifaa hivyo kwa sababu ya hupenda kusikiliza muziki hasa kutoka kwenye simu yake.

Pia kwa upande wake Rajabu Nahemia mkazi wa Tabata Dar es Salaam, anasema anapenda kutumia earphone kwa sababu hapendi kusikiliza muziki mbele za watu, kwani muda huo huwa kwenye hisia fulani.

Mbali na kupenda muziki amesema anavaa earphone ili aweze kupata ‘testi’ ya muziki anaosikiliza na wakati mwingine anazivaa kwa ajili ya fasheni.

Licha ya watumiaji wa vifaa hivi kuwa na sababu mbalimbali za kuvitumia, Dk Bukanu amesema uvaaji wa earphone kwa muda mrefu ni hatari kwa afya ya masikio kwani kunaweza kuharibu uwezo wa kusikia.

Aidha ameshauri watu kutotumia earphone na kama zikiwa na ulazima wanatakiwa kutumia kwa sauti ya chini sana, ambayo haitazuia watu wanaozungumza pembeni kutosikika kwa sababu sauti kubwa huleta athari kubwa kwa masikio.

Mbali na kusababisha matatizo ya masikio Banaku ameongeza, "Uvaaji wa vifaa hivyo haushauriwi sana kwa sababu pia huweza kusabababisha ajali kwa mtumiaji endapo akiwa barabarani kwa kutosikia vitu vya pembeni yake."

Ameeleza kuwa wapo watu wengi wanaopata shida ya masikio, ambao mara nyingi hupatiwa msaada wa mashine ya usikivu ambazo huwa zinakuza sauti ili waweze kusikia.

Banaki amemaliza kwa kusema upataji wa matatizo ya masikio haujalishi mtu ametumia earphone kwa siku ngapi au muda gani, kwani kuna mtu anaweza kutumia kwa siku moja lakini kwa sauti ya juu pia anaweza kupoteza uwezo wa kusikia.

Dk Mfuko pia aliongeza kuwa wanapofanya vipimo huweza kubaini ni namna gani mgonjwa alipata tatizo, iwapo ni kusikiliza sauti kubwa au maambukizi ya fangasi au bakteria.

Licha ya ushauri ambao umetolewa na daktari huyo, kampuni zinazotengeneza vifaa hivyo pia zimekuwa zikijali afya za wateja wao kwa kuweka teknolojia ambayo msikilizaji akiwa anasikiliza muziki kwa sauti ya juu zaidi ya asilimia 50, vifaa hivyo hujishusha sauti na kutoa tahadhari kwa mtumiaji






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post