Ukweli kuhusu msemo wanaogombea Shafii Brand, Steve Mweusi

Ukweli kuhusu msemo wanaogombea Shafii Brand, Steve Mweusi

Kufuatia mvutano wa kugombania msemo unaofanania na "Kuchekacheka tu kuoga aaah" kati ya wachekeshaji Shafii Brand na Steve Moses 'Stive Mweusi', Ofisa Usajili kutoka Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni 'Brela', Stanslaus ameeleza kuwa kwa kawaida mtu anayefika wa kwanza kusajili msemo au kauli mbiu ndiye hutambulika kama mmiliki halali wa msemo huo.

"Anayefika wa kwanza ndiye ambaye tunaamini ni mmiliki halali kwa hiyo kama kuna jambo la kubishania maana yake hapo litafunguliwa shauri, kuna jambo moja ambalo natamani lifahamike Brela ni Ofisi ya Msajili wa Alama na Huduma ni kama mahakama tu kwa hiyo kuna kesi fulani zinaletwa na zinasikilizwa zinazohusi migogoro ya umiliki wa biashara na huduma kwa hiyo kama kuna jambo ambalo linabishaniwa na pande mbili basi linafunguliwa shauri hapahapa na linasikilizwa na kutolewa uamuzi upande ambao utakuwa haujalidhika na uamuzi ambao umetolewa na msajili basi na kuna nafasi ya kwenda mahakamani kwa ajili ya kukata rufaa,"amesema.

Stanslaus ameyasema hayo leo Jumanne, Julai 2, wakati akizungumza na Mwananchi na kuongeze kuwa mmiliki ili apate ulizi wa kisheria wa msemo, kauli mbiu ni lazima awe ameusajili.

"Mmiliki ili apate ulizi wa kisheria wa huo msemo lazima awe ameusajili kama alama ya biashara hivyo kila msanii anapokuwa na msemo ambao anautumia kwenye kazi zake za biashara ya sanaa au hatakama siyo sanaa anaweza kuusajili kama alama ya biashara kutegemeana na huduma anayoitoa,"amesema.

Hata hivyo, ameeleza taratibu za kufuata ili mtu aweze kufanya usajili wa msemo, kauli mbiu au biashara yake kupitia njia ya mtandao.

"Taratibu za kusajili zinapatikana kwenye njia ya mtandao kwa hiyo mtu anayetaka kusajili msemo wake au kauli mbiu atasajili kupitia mfumo wetu unaopatikana kwa njia ya mtandao malipo yamegawanyika katika awamu mbili, awamu ya kwanza mmiliki wa msemo anatuma maombi ya kuomba kusajili ambayo ni Sh 65,000 kwa maana ya kwamba, atalipa Sh 50,000 kama ada ya maombi alafu Sh 15000 atalipa kama ada ya kutangaza huo msemo kwenye jarida letu ambalo linatoka kila mwezi.

"Lengo la kuchapisha kwenye hilo jarida ni jamii iweze kusoma na kuona ili kama kuna mtu anatumia hiyo alama au msemo aweze kuweka pingamizi na kama kutakuwa hakuna pingamizi ndani ya siku 60 atakayekuwa ameleta maombi ya usajili anaweza kutuma kwa njia ya mtandao kwa msajili wa alama za biashara na huduma ili aweze kumpatia cheti cha usajili ambacho nacho atalipia Sh 65000, ambapo Sh 60000 kama maombi ya kupata cheti cha usajili na Sh 5000 ni ada ya mwaka", amesema.

Utakumbuka kuwa hivi karibu imezuka sintofahamu ya kudaiana msemo kati ya wachekeshaji hao wawili huku kila mmoja akidai kuwa ni wake. Mbali na wawili hao mchekeshaji  Theodoro Emmanuel 'Kago' mwishoni mwa mwaka jana  alimtuhumu mwanamuziki wa Bongo Fleva Mavokali kutumia msemo wake bila ya kuomba ruhusa na kisha baadaye wakamaliza tofauti zao.

Aidha mwaka 2020 mwanamuziki wa Bongo Fleva Khalid Mohamed 'TID' aliwahi kulalamika na kudai kuwa msemo wake 'Ni Yeye' umetumika kwenye kampeni za kisiasa za Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema bila ya ruhusa yake.
.
.
.
#MwananchiScoop
#Burudika Nasi






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Christina Lucas


Latest Post