Snura: Nimeacha muziki, nikifa msiniposti

Snura: Nimeacha muziki, nikifa msiniposti

Mwanamuziki Snura Mushi ametangaza kuacha muziki huku akikataza nyimbo zake kupigwa tena kwenye vyombo vya habari. Hatua hiyo imekuja baada msanii huyo kudai amemrudia Mungu.

"Watanzania na nje ya nchi mimi Snura leo natangaza rasmi kuwa nimeacha kazi za sanaa nilizokuwa nazifanya. Sababu kubwa ya kuacha ni kumrudia muumba wangu, nifate dini yangu ya Kiislamu inavyosema mwanamke wa Kiislamu anavyotakiwa kuwa," amesema.

Mbali na hilo, msanii huyo amesema anajutia aliyokuwa akiyafanya kipindi akiwa kwenye sanaa.

"Nisiwe muongo najutia sana niliyoyafanya na maamuzi yangu niliyafanya miaka mingi iliyopita, mwanzoni wazo langu lilikuwa kuacha kimyakimya nisiseme kwa yeyote wala popote ijue tu familia yangu, ndugu zangu na watu wanaonizunguka lakini kwa sababu hivi vitu vinaishi miaka na miaka na vizazi vipya vinakuja sitaki kuwa sababu ya kuwaharibu," amesema.

Katika hatua hiyo ya kutangaza kuacha muziki pia ameomba nyimbo zake kuacha kupigwa kwenye vyombo vya habari. 

"Nikaona kuna sehemu ambayo mimi naweza kusikilizwa kwenye redio, Tv na kawaida najua ni watu waelewa sana na kitu ninachomshukuru nisingeweza kupita kila redio na Tv kuwakataza wasicheze nyimbo zangu, natumia fursa hii ndugu zangu kwa heshima na taadhima naomba sana mnipokelee ombi langu msicheze kazi zangu kabisa naomba mfute fanyeni kama hakuna kilichotokea," amesema Snura.

Licha ya kukataza kazi zake kuchezwa kwenye vyombo vya habari pia amekataza picha zake kuchapishwa kwenye mitandao ya kijamii siku atayofariki dunia.

"Ukisikia nimekufa umehuzunishwa na msiba wangu njoo unizike kama ni mwanamke usije mtupu njoo na stara, picha ambazo hazina heshima msiposti hayo mapicha wala madude dude kwa sababu naona tukifa hayo madude ndiyo mnaposti," amesema.

Utakumbuka kuwa Sura aliwahi kutamba na ngoma kama vile Majanga, Nimevurugwa, Chura, Shoga Yake Mama, Ushaharibu, Shindu na nyinginezo.

Hii itakuwa si mara ya kwanza kwa msanii kutangaza kuachana na kazi za sanaa na kumrudia Mungu. Mwaka 2016 Mzee Yusuph aliwahi kutangaza kuacha muziki na kurudi kumtumikia Mungu, lakini mwaka 2020 alirudi tena kuimba muziki.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Christina Lucas


Latest Post