Sintofahamu yatokea mahakamani, kesi ya Diddy

Sintofahamu yatokea mahakamani, kesi ya Diddy


Mahakama Kuu ya Shirikisho mjini Manhattan, Marekani, iliendelea kushuhudia drama za aina yake katika kesi ya nyota wa muziki Sean “Diddy” Combs, ambaye anakabiliwa na mashItaka mazito ya usafirishaji wa kingono na mengineyo.

Juni 15, hali ya sintofahamu iliibuka mahakamani baada ya mawakili wake kuwasilisha barua rasmi kwa Hakimu Arun Subramanian wakitaka kesi isitishwe endapo mmoja wa wajumbe wa baraza la majaji ‘Juror’ ataondolewa mahakamani.

Wanasheria wa Diddy walidai kuwa jaribio la kutaka kumuondoa Juror No 6 ambaye ni Mmarekani mweusi, linaonyesha upendeleo na linaweza kuathiri haki ya mteja wao kupata uamuzi wa haki, ambapo wakili mkuu wa Diddy alieleza kuwa kama juror huyo ataondolewa, watalazimika kuomba “mistrial”, yaani kesi ianze upya kwa sababu ya ukiukwaji wa haki za msingi.

Wiki iliyokwisha jaji wa mahakama alitishia kumuondoa Juror mmoja mahakamani baada ya kudaiwa kuwa na mawasiliano yasiofaa na wenzake pamoja na upendeleo jambo ambalo mawakili wa Diddy walipinga hilo lisifanyike.

Endapo pingamizi la mawakili wa Diddy litakubaliwa, inaweza kuwa pigo kubwa kwa upande wa mashtaka na kuchelewesha haki kwa wahanga wanaodai kudhulumiwa na msanii huyo.

Aidha kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya mahakama, upande wa mashtaka unakaribia kukamilisha ushahidi wake kabla ya wiki ya sita kuisha huku ikiwa na maana kuwa muda si mrefu upande wa Diddy utaanza kuwasilisha hoja zake.

Mpaka kufikia sasa zaidi ya mashahidi 18 tayari wametoa ushahidi wao akiwemo aliyekuwa mpenzi wa zamani wa Diddy, Cassie Ventura (Cassie), Jane (Ex wa Diddy), Kid Cudi, Mia, Capricorn Clark, Kerry Morgan, Bryana Bongolan na wengineo.

Diddy anakabiliwa na mashtaka ya usafirishaji wa binadamu kwa ajili ya ngono, njama ya kihalifu (racketeering), na usafirishaji kwa lengo la kushiriki katika ukahaba. Amekana mashitaka yote na endapo atapatikana na hatia, anaweza kuhukumiwa kifungo cha maisha gerezani.

Utakumbuka Sean "Diddy" Combs alikamatwa Septemba 16, 2024 katika hoteli ya Park Hyatt, Manhattan, New York na kupelekwa moja kwa moja katika gereza la Metropolitan huko Brooklyn. Kesi yake ilianza kuzikilizwa Mei 5,2025.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post

Latest Tags