Majibu ya Shilole kuhusu kuvunjika kwa ndoa yake

Majibu ya Shilole kuhusu kuvunjika kwa ndoa yake

Vipi, wameachana au ni kiki? maswali ni mengi kwa ndoa ya msanii na mfanyabiashara Zuwena Mohamed 'Shilole' na mumewe Rajabu Issa 'Rommy' kutokana na yanayoendelea mitandaoni.

Wawili hao ambao walifunga ndoa Aprili 22, 2021 wameacha maswali kwa mashabiki tangu jana kutokana na yanayozungumzwa kwenye mitandao ya kijamii huku wengine wakidai ni kiki kwani 'Shishi' anataka kuachia wimbo mpya.

Hata hivyo, watu wa karibu wa wawili hao wamesema chanzo cha kuvunjika kwa ndoa hiyo ni wivu wa kimapenzi na Rommy anadai Shilole anachepuka.

Kwenye mitandao ya kijamii kuna video inayomwonyesha Shilole akiwa na mwanaume wamekaa kwa ukaribu huku mezani kukiwa na vinywaji na inadaiwa mwanamume huyo ndiye anayehusishwa anatoka kimapenzi na msanii huyo anayetesa na nyimbo kama 'Kisasa', 'Viuno', 'Mama Ntilie', 'Pindua Meza' na nyingine nyingi.

Mwananchi lilimtafuta msanii huyo ambaye pia anamiliki mgahawa maarufu wa kuuza chakula la vinywaji wa Shishi Food ili kuthibitisha taarifa hizo za kuvunjika kwa ndoa yake na kudai muda wa kuongelea jambo hilo haujafika na atalizungumzia upepo ukitulia.

"Aise sitaki kupokea simu za watu wengi maana nikipokea tu swali linalokuja ni tumeaachana na Rommy. Hivyo, sitaweza kuzungumza kwa sasa, niache kwanza huu upepo upite," amesema Shilole.

Mwananchi iligeukia upande wa pili kwa mume wa Shilole 'Rommy' na alipopigiwa simu, iliita bila kupokelewa.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye, Rommy alituma ujumbe kwenye ukurasa wake wa Whatsapp na haya ndiyo aliyoandika;

"Habari.....Ndugu zangu kama ambavyo mmeona kwenye mitandao na hiyo ndiyo hali halisi basi mimi na aliyekuwa mwenzangu Zuwena Mohamed (Shilole) naona tumefikia mwisho na si vibaya nikakubali matokeo na kumpisha kijana mwenzangu aendeleze gurudumu hili, na maisha yaendelee... nipende kutoa shukrani zangu za dhati kwa vile tulivyoishi siku zote za mapenzi yetu . Wabillah Tawfiq."

Baada ya kuchapisha ujumbe huo, watu walimjibu kwenye 'Comment' wakimpa pole, huku wengine wakiona ni kiki kwa sababu Shilole anataka kutoa wimbo mpya kwani ni muda mrefu hajasikika kwenye muziki.

Richi Mitindo 'Mume wa Jackline Wolper' aliandika, "Habari mbaya kusikia. Isiwe kweli labda dada Shishi aachie hiyo nyimbo."

Kondo1183 aliandika "Shishi hanaga kiki kwenye muziki wake, ila pia wengi tunaomba isiwe kweli na ikiwa kweli ni aibu kubwa kwa Shishi kwann hadumu na wanaume wake shida nini?"

Kabla ya ndoa hiyo, Shilole alikuwa kwenye ndoa na Ashraf Uchebe Desemba 2017 na waliachana kwa madai ya kuchoshwa na vipigo vya muda mrefu   kutoka kwa mwanamume huyo.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post