Kama unataka ndoa imara olewa na mwanaume kama baba yako

Kama unataka ndoa imara olewa na mwanaume kama baba yako

Onyo: Ushauri huu unawahusu tu wale ambao walikuwa na uhusiano mzuri na baba zao.

Kama unampenda baba yako na uko au ulikuwa na uhusiano naye mkawa kama marafiki, endelea kusoma ushauri wangu, lakini kama baba yako alikuwa ni mnyanyasaji mlevi kupindukia na asiyejali familia na hukuwahi kumpenda wala kuwa na uhusiano naye kama baba na rafiki mwema kwako, naomba usipoteze muda wako kusoma ushauri wangu..

  1. Atakulinda na utajisikia kuwa salama kuwa naye:

Kama mpenzi uliyempata atakuwa na tabia zinazofanana na baba yako kwa kiasi cha kutosha, utajisikia uko salama kuwa naye karibu. Kwa asili wanawake wote hupenda kujiona wako salama pale wanapokuwa na wapenzi wao kabla hata ya kuingia kwenye ndoa, hivyo kwa kuhakikishiwa usalama na mpenzi wako kama alivyokuwa akifanya baba yako, ni dalili nzuri kwamba umempata mume wa maisha yako.

  1. Unajua namna ya kuishi naye na kudumisha ndoa yenu:

Ulikuwa unamuona mama yako jinsi alivyokuwa akimfanyia baba yako.

Unajua kwa usahihi kabisa jinsi walivyokuwa wakiishi na namna wanavyochukuliana. Kwa uzoefu ulioupata kutoka kwa mama yako jinsi alivyokuwa akiishi na baba yako, naamini utakuwa kwenye nasafi nzuri ya kudumisha upendo katika ndoa yenu.

Utakuwa unajua ni eneo gani anapenda kusifiwa, utakuwa unajua ni mambo gani huwa yanamkera, unajuwa ni wakati gani huwa anapenda kuachwa peke yake akitafakari mambo yake na unajua ni wakati gani anahitaji kuliwazwa na kubembelezwa…

  1. Utakuwa unajua vitu vinavyomsababishia msongo wa mawazo:

Kama utamuona mpenzi wako kila akija nyumbani kwenu huzungumza na baba yako kuhusu maisha na changamoto zake pamoja na mambo mengine yanayohusiana na familia, basi hapo unaweza kutabiri kwa usahihi kabisa kwamba, ni maeneo gani yanampa hofu mpenzi wako katika maisha na ni maeneo gani anahitaji kupewa moyo na msaada wa mawazo.

  1. Utakuwa na nafasi ya kuongeza kiwango cha elimu:

Inawezekana baba yako alikuwa anakushauri sana kusomea taaluma kama yake na kufikia kiwango cha elimu kama chake na pengine alikuwa anapenda sana kukutolea mifano ya wanandoa kadhaa waliopata mafanikio katika ndoa zao ambao wamesomea taaluma kama yake, kwa hiyo kama mpenzi wako ana ndoto kama za baba yako na mazungumzo yake na mipango yake inafanana na ya baba yako basi ujue kwamba, utakuwa na nafasi nzuri ya kuongeza kiwango chako cha elimu kwa kadiri upendavyo.

  1. Utakuwa huru kusema hisia zako pale unapokwazika:

Inawezekana ulikuwa huogopi kuzungumza kwa uchungu au kulazimisha kutatuliwa tatizo lako na baba yako hususan pale unapoona kwamba, matakwa yako hayakufuatwa au kusikilizwa. Kama ukiudhiwa na jambo unazungumza bila woga, na kama ulikuwa ukihisi kutotendewa haki katika jambo, ulikuwa ukizungumza kwa uhuru bila woga, basi kama mpenzi wako anafanana kitabia kwa asilimia kuwa na baba yako, ujue kwamba, utakuwa na huru kusema hisia zako bila woga katika ndoa yenu. Kwa hiyo katika eneo hilo la mawasiliano kakika ndoa litakuwa limekamilika.

  1. Hata baba yako atampenda:

Mara nyingi wazazi wengi wa kiume wanaowapenda mabinti zao huwalinda sana, hivyo hutaka kuona mabinti zao wakiangukia katika mikono salama. Kama baba yako na mpenzi wako kuna mambo kadhaa wanaendana, hiyo itakuwa ni karata nzuri itakayomshawishi baba yako asiweke vikwazo katika kuolewa kwako, kwa sababu ana uhakika kwamba, utakuwa kwenye mikono salama.

  1. Hata mama yako naye pia atampenda:

Duh, kwa upande wa mama yako ndio usiseme maana kila akimuona mpenzi wako atakuwa anamfurahia kama vile alivyokuwa akifurahi kila wanapoonana na baba yako, enzi zao walipokuwa wakiposana.

  1. Unaweza kutabiri kwa usahihi kabisa kwamba atakuwaje pindi atakapo kuwa mtu mzima:

Je unataka kujua maisha yenu ya ndoa yatakuwaje baada ya miaka kumi, ishirini, thelathini ya ndoa? Ukitaka kujua hilo, chunguza maisha ya ndoa ya wazazi wako, utapata jibu.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Shaban Kaluse

A Sales and Marketing in the hospitality Industry and also a freelance journalist, writing about love and relationships and educative articles which aims for youths, every Tuesday on Mwananchi Scoop.


Latest Post