Baba Asma Wa Dunia Hazitaki Tv Anaridhishwa Na Digitali

Baba Asma Wa Dunia Hazitaki Tv Anaridhishwa Na Digitali

Mtayarishaji na Muongozaji wa Tamthilia inayofanya vizuri katika mtandao wa YouTube ya ‘Dunia’ Issa Madinga maarufu Baba Asma ameweka wazi kukataa mapendekezo kadhaa kutoka kwa wamiliki wa TV kutokana na imani yake kuwa kwenye digital.

Akizungumza na Mwananchi, Baba Asma ameeleza kuwa zipo Telev
isheni nyingi ambazo zimeomba kufanya naye kazi lakini amekataa kwani yeye na waigizaji wake wamechagua kuwekeza nguvu mitandaoni.
"Chanzo chetu kikubwa cha mapato ni Youtube kwa maana ya mitandao ya kijamii kama kazi ikiwa nzuri tunapata hela japo sio kwamba tunapata sana lakini tunaishi na wasanii wetu wote wanalipwa kupitia Youtube lakini matangazo yapo na yanaongezea pato kidogo lakini chanzo chetu kikubwa cha kipato ni Youtube" amesema Baba Asma.

Muongozaji huyo amesema hayupo tayari kuingia ubia na kampuni yoyote ya televisheni ili kuirusha tamthilia yake, akisema kuwa anaamini kwenye mitandao kwa sababu ya kufikia watazamaji wengi lakini pia kwenda na kasi ya ulimwengu wa teknolojia.

“Zipo baadhi ya Televisheni ambazo zimeomba kufanya kazi nasi, kwasababu tamthilia ni kubwa na inafanya vizuri lakini kwa bahati mbaya sivutiwi na TV, mimi ni mtu ambaye naamini sana kwenye majukwaa ya kidigitali, kwasababu naamini ndio usasa zaidi lakini pia naweza kufikia watazamaji wengi zaidi kuliko kwenye Televisheni na ukiangalia ulimwengu sasa umehamia kiganjani kwa hiyo minaamini kwenye Digital Platform," amesema Baba Asmah.

Aidha, ameweka wazi namna ambavyo anawapata waigizaji wa tamthilia yake ya Dunia, akisema kuwa yupo kwenye gemu kwa muda mrefu hivo hukutana nao kwa njia tofauti tofauti.

“Kwa sababu mimi ni mtu wa sanaa kwa muda mrefu kidogo karibu miaka minne kwa hiyo muda mwingine huwa yanakuja maombi ya watu wanataka kuigiza, kuna wengine nawatafuta, muda mwingine kama nahitaji msanii mkali kuna watu wananiunganisha nao kwa hiyo huwa nawapata kwa namna hiyo," amesema Baba Asma.

Hata hivyo, ameeleza sababu za kwanini mmoja wa waigizaji wa tamthilia ya Dunia, Matilda kutoonekana kwenye tamthilia hiyo hivi karibuni.

“Mati amepata shida kidogo ya kiafya, ni muda mrefu tulikuwa tunajitahidi kwenda naye hata watazamaji wakiangalia vizuri baadhi ya Episode za mwishoni mwishoni alikuwa anaonekana kabisa hayupo sawa, lakini ikaenda hospitali na daktari akasema inabidi apumzike hakuna namna maana tulikuwa tunapambana hata yeye mwenyewe alikuwa hataki kwa hiyo tulikuwa tumechanganyikiwa kiufupi.

"Lakini ikawa hakuna jinsi yule ni binadamu kapata shida kwa hiyo inabidi apumzike karibu miezi minne mpaka sita, tukaona hatuwezi kusimama kufanya kazi kwa sababu project hii ni kubwa sana kuliko msanii, na kuna wasanii wengi ambao bado wanawakilisha, lakini pia watazamaji hatuwezi kuwanyima hii burudani na hatuwezi kubadilisha stori kwa hiyo ilibidi atafutwe mbadala wake," amesema Baba Asmah.

Pia, amekanusha taarifa zilizosambaa kwenye mitandao ya kijamii zikisema kuwa sababu ya Matilda kutoonekana kwenye tamthilia hiyo ni kutokana na masuala ya kimkataba na uongozi wa tamthilia hiyo.

“Hapana sio kweli, unajua hizo taarifa zinatokea lakini bahati nzuri pia na yeye aliamua ku-clear na alifanya video kabisa akizungumzia kuwa hayupo sawa anaumwa kwa hiyo yupo mapumzikoni na kuhusu kujiposti anachoumwa na kwamba hawezi kusimama kwa muda mrefu, hawezi kufanya kazi ngumu kwa hiyo anahitaji kukaa nyumbani na kupumzika, sio kwamba yupo mahututi hawezi kusimama, hapana," amesema Baba Asmah.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Masoud Kofii


Latest Post

Latest Tags