Uhusika wa filamu ulivyohatarisha maisha ya waigizaji

Uhusika wa filamu ulivyohatarisha maisha ya waigizaji

Kila kazi huna na changamoto zake, bila kujali ukubwa au udogo wake. Katika tasnia ya uigizaji wasanii hutumia mbinu mbalimbali ili kuzipa ubora kazi zao, lakini mbinu hizo wakati mwingine huwasababishia matatizo.

Kati ya mbinu kubwa wanayotumia ni kuuvaa uhusika na kuutendea haki kulingana na ‘script’ inavyotaka. Katika kufanikisha hilo wapo ambao wamewahi kupata matatizo ya kiafya kama vile kuvunjika wakati wakipika kazi hizo za sanaa.

Hawa ni baadhi ya waigizaji waliowahi kupata matatizo ya kiafya wakati wakijaribu kutendea haki uhusika wa filamu.

1. Jackie Chan
Mwigizaji Jackie Chan kutoka Hong Kong ambaye wengi wamekuwa wakivutiwa na kazi zake, kutokana na uvaaji wake wa uhusika ni kati ya waigizaji waliowahi kupata majeraha mengi akiwa kazini.

Majeraha hayo ni pamoja na kuvunjika viungo na maumivu ya misuli.
Amewahi kueleza kuhusu majeraha hayo katika mahojiano mbalimbali na kwenye vitabu vyake kama kile cha “I Am Jackie Chan” na kwenye vipindi mbalimbali amekuwa akizungumzia kazi yake na hatari alizowahi kukumbana nazo.

2. Tom Cruise
Katika filamu kama “Mission Impossible,” mwigizaji Tom Cruise kutokana na uhusika aliokuwa nao ulipelekea avunjike goti wakati akiruka kutoka jengo moja hadi lingine.

Mwigizaji huyo akiwa kwenye kipindi cha “The Graham Norton Show” na katika mahojiano na “Jimmy Kimmel Live!” amewahi kueleza kuhusu majeraha aliyoyapata.

Hakuacha kuzungumzia tukio lake la kuvunjika goti wakati wa kuruka kutoka jengo moja hadi lingine, aidha alizungumzia jinsi majeraha hayo yalivyomlazimu kuendelea kufanya kazi licha ya maumivu aliyokuwa nayo.

3. Charlize Theron
Mwigizaji Charlize Theron ambaye alijibadilisha mwonekanao kwa kiasi kikubwa kwa ajili ya uhusika wake katika filamu ya “Monster,” alijikuta akipata majeraha ya muda mrefu kutokana na mabadiliko ya mwili aliyofanya.

Charlize akiwa kwenye mahojiano na jarida la Allure aliwahi kueleza jinsi alivyokabiliwa na majeraha wakati wa kurekodi filamu yake ya Monster ambayo alivaa uhusika wa Aileen Wuornos.

Katika filamu hiyo alilazimika kubadilisha mwili wake kwa kiwango kikubwa, kupungua uzito na mabadiliko mengine ambayo yalimfanya ahisi maumivu na uchovu kwa muda mrefu.

4. Halle Berry
Naye mwigizaji Halle Berry alikumbana na majeraha kadhaa wakati wa kurekodi filamu kama “Die Another Day,” ambapo alipata majeraha ya mkono yaliyomuathiri kazi yake kwa muda mrefu.
Amewahi kueleza kuhusu majeraha hayo wakati akifanyiwa mahojiano kwenye red carpet ya tukio la uzinduzi wa filamu ya “Die Another Day” mwaka 2002.

5. Daniel Craig
Daniel Craig katika filamu ya “Skyfall,” alijeruhiwa mguu wake jambo lililomlazimu afanyiwe upasuaji.

Aliwahi kuzungumzia majeraha hayo wakati wa mahojiano na vyombo vya habari na pia kwenye red carpet ya uzinduzi wa filamu ya “Skyfall.”

6. Keanu Reeves
Mwigizaji Keanu Reeves kutokana na uhusika wake kwenye filamu ya “John Wick,” ulimfanya apate majeraha mbalimbali, ikiwa ni pamoja na maumivu ya misuli na mguu.

Keanu Reeves amekuwa akizungumza kuhusu majeraha aliyopata wakati akicheza filamu ya “John Wick.” ikiwemo majeraha ya mguu na kidole.

Wakati akifanyiwa mahojiano kwenye uzinduzi wa filamu hiyo alisema kazi ya uigizaji inahitaji kujitolea

Hayo yote yanaenda sambamba na tukio lililowahi kutokea mwaka 1993 la mwigizaji wa zamani Brandon Lee kufariki dunia wakati akiigiza filamu ya ‘The Crow’.

Kifo chake kilitokana na kupigwa risasi kwa bunduki iliyoonekana kuwa salama kwa maigizo bila ya kujua kuwa ilikuwa na risasi iliyobaki kwa bahati mbaya.

Tukio hilo lilikuwa na athari kubwa kwenye tasnia ya filamu na lilisababisha mabadiliko katika sheria za usalama wa silaha katika uzalishaji wa filamu. Ikumbukwe kuwa Brandon Lee alikuwa mtoto wa mwigizaji maarufu Bruce Lee.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Christina Lucas


Latest Post