Penzi la Katy Perry na Bloom lakalia kuti kavu

Penzi la Katy Perry na Bloom lakalia kuti kavu


Uhusiano wa mwimbaji wa Pop Marekani, Katy Perry, 40, na mchumbaji wake, Orlando Bloom, 48, ambaye ni mwingizaji wa Uingereza unatajwa kukalia kuti kuvu huku kisirani cha mrembo huyo kikitajwa kuwa ndio chanzo cha hayo yote.

Chanzo kimoja kimeuambia mtandao wa Page Six kuwa mastaa hao wamefikia hatua ya kuachana na kichosubiriwa ni kumalizika kwa ziara ya Katy Perry 'Lifetimes' iliyoanza Aprili 23 na inatarajiwa kukamilika Desemba 7 mwaka huu.

Ikumbukwe wawili walikutana kwa mara ya kwanza Januari 2016 kwenye tafrija ya baada ya sherehe ya Golden Globes kisha ukurasa mpya baina yao ukaanza lakini mnamo Februari 2017 walithibitisha kwamba walikuwa wametengana.

Perry, mkali wa kibao, Roar (2013) ambacho video yake imetazamwa YouTube zaidi ya mara bilioni 4.1, alianza tena uhusiano na Bloom mnamo Februari 2018, na wakachumbiana Siku ya Wapendanao 2019.

Wakati mashabiki wakishangazwa na mambo yao, Machi mwaka uliofuatia wakatangaza kutarajia mtoto wao wa kwanza ambaye Perry alikuja kujifungua mtoto wa kike hapo Agosti 26, 2020 na kumpa jina la Daisy Dove.

"Kila kitu kimemalizika, wanasubiri hadi ziara yake [Katy Perry] ya Lifetimes iishe ndipo watengane," Page Six, safu ya udaku ya gazeti la The New York Post ilinukuu chanzo kimoja kilicho karibu na mastaa hao.

Hata hivyo, mtandao wa People unadai kuwa Perry ana msongo wa mawazo unaotokana na kupokelewa vibaya kwa albamu yake mpya na ya saba, 143 (2024), jambo ambalo ndilo hasa limeleta mvutano katika uhusiano wao.

"Katy Perry alikuwa na hasira pamoja kisirani sana baada ya kupokea matokeo mabaya kuhusu albamu yake mpya. Ilimfanya awe na msongo mwingi wa mawazo. Bloom alimwelewa, lakini hilo lilisababisha mvutano."

"Vilevile alikuwa amesikitishwa na baadhi ya makadirio ya ziara yake kutotimia kama walivyotegemea, hilo limeongeza msongo kwenye uhusiano wao." vyanzo hivyo vilitaja hayo kama chanzo cha mgogoro wao.

Mwaka uliopita kwenye kipindi cha Call Her Daddy, Perry alizungumzia mgogoro wao wa zamani na kusema awali walikuwa hawajajitoa kikamilifu katika uhusiano wao hasa yeye ingawa Bloom alionyesha nia ya kufika sehemu.

"Nilikuwa nimetoka tu kwenye uhusiano mwingine, na nilijisikia kama siwezi tena kuwa peke yangu. Nilihitaji kubadilika, nilihitaji kiota kipya lakini nililazimika kufanya kazi kubwa ya kujirekebisha." alisema Perry.

Mwezi huo huo, Perry akiongea na People alisema, "Mimi na Bloom, tunapogombana, tunapigana kwa nguvu na haraka, kisha tunapatana upesi. Ni kama, 'La la la la la, nakupenda. Sawa, tuendelee."

Kwa upande wake Bloom, staa wa filamu 'Pirates of the Caribbean', mwaka 2023, alizungumzia changamoto zao na kusema wapo katika faini tofauti, yaani filamu na muziki na hakuna anayeijua ya mwenzake vizuri na ndipo mgongano wao unapoanzia.

"Wakati mwingine mambo yanaweza kuwa magumu sana lakini sitakubali. Sisi hupambana na hisia zetu na kazi zetu. Sote tunatambua jinsi tulivyo na bahati kwa kuwa tumeunganishwa kwa njia ya kipekee, hivyo hakuna nafasi ya kukata tamaa," alisema Bloom.

Ikumbukwe Katy Perry aliyevuma na kibao chake, Dark Horse (2013), alitajwa na Billboard kama mwanamuziki wa kike aliyelipwa fedha nyingi zaidi duniani mwaka 2015 na 2018, pia kuwa mmoja wa wasanii wakubwa wa pop wa karne ya 21.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post

Latest Tags