Ndaro ataka kuwa kama Mwamposa, atoboa siri njia atazotumia

Ndaro ataka kuwa kama Mwamposa, atoboa siri njia atazotumia

 

Ukurasa wake mpya wa maisha ya umaarufu ulianzia baada ya kusimamia kipajike cha uchekeshaji, baada ya kuachana na kazi ya uwalimu aliyokuwa akiifanya mwanzo. Huyu si mwingine ni Masatu Amoni Ndaro kwa jina la umaarufu Ndaro.

Jarida la Mwananchi Scoop limepata wasaa wa kufanya mahojiano  na Ndaro ambaye wengi wanamuita Mjeshi Kikofia na kuelezea maisha yake kutoka kwenye Ualimu mpaka kuingia katika sanaa ya vichekesho.

 

Alijiripua kuingia kwenye uchekeshaji

 Ndaro ameeleza kuwa haikuwa kazi rahisi kuingia katika sanaa, kipindi anaishi Kigoma na wazazi wake

 ilibidi amdanganye baba yake kuwa amepata kazi nyingine ya kufundisha Dar es salaam yenye maslahi makubwa.

“Aisee haikuwa kazi rahisi kwangu mpaka hivi leo kwa sababu kuingia katika sanaa ya vichekesho nilijiripua kwa kumshawishi na kumdanganya baba yangu kuwa naenda Dar kufanya kazi yangu ya ualimu, basi niliruhusiwa kuja Dar huku akili yangu ikiwaza kufanya vichekesho, lakini hali ilikuwa ngumu sana marafiki zangu walikuwa wananisaidia kuendesha maisha kwa muda huo” anasema Ndaro.

 

ATAMANI KUWA KAMA MWAMPOSA

Msanii huyo ameeleza kuwa shauku yake kubwa anatamani kuwa kama mchungaji Mwamposa kutokana na mchungaji huyo kujijengea imani kwa waumini wake kwa sababu ya ushawishi aliyonao.

 

“ Natamani siku moja niwe na nguvu ya ushawishi kama Mwamposa nakuaminika kwa watu na ndiyo vitu nilivyopanga kuvifanya katika huu mwaka cha kuwahakikishia watu nitafanya kazi sana na kusali ili nifike ‘levo’ ya Mwamposa.

Nataka ikifika mwezi Disemba tuwe tunaongea mengine kuhusu mimi nitaingia hata kwenye maswala ya imani hata kuimba gospel nitafanya hivyo ilimradi nifikie lengo” anasema Ndaro

 

Harakati za kufika Cheka Tu

Siku zote waswahili wanasema penye nia pana njia, baada ya Ndaro kufika Dar es salaam na kuhangaika huku na kule kukuza kipaji chake mwaka 2021 aliweza kushiriki mashindao ya Cheka Tu Search.

Kipindi ambacho Cheka Tu inatafuta vipaji vya kuchekesha Ndaro hakufanya ajizi kwenda na kuonesha kipaji chake, japo haikuwa rahisi baada ya Audition ya kwanza kuanza Mwanza. Ambapo ilibidi afunge safari kwenda kwenye mkoa huo, lacha ya kuwa hakufanikiwa kwa muda huo.

Baada ya kurudia tena kwenye mashindano hao bila kukata tamaa hatimaye alipita nafasi na kufanikiwa kuwa mshindi wa tano, ambapo mshindi wa kwanza alikuwa kutoka Dar es salaam.

“ Unajua ukitaka kufanya jambo lazima ujitafute sana tu na kama umeandikiwa utakipata kwa muda wowote nilifanikiwa kuingia katika mashindano ya kusaka vipaji vya kuchekesha na kuwa mshindi wa tano.

Japo ningekuwa nimekata tamaa nisingefika hapa nilipo kwa maana mara ya kwanza ilikuwa ngumu kuingia kwenye mashindano lakini mara ya pili nilipojaribu tena nikafanikiwa”. Anasema Ndaro

Baada ya kuwa mwanafamilia wa Cheka Tu inayomilikiwa na Coy Mzungu, Ndaro alihisi mafanikio yatakuja kwa haraka yaani alikuwa anaona tayari amekuwa tajiri.

 

“Mara ya kwanza napanda ‘stejini’ kutokana na lile vibe la watu kunikubali tayari akili yangu ilikuwa inaniambia nitakuwa na pesa nyingi nitamiliki nyumba na magari kwa haraka kumbe mambo yalikuwa tofauti na kwamba Cheka tu ni daraja la kwenda kujitafuta sehemu nyengine” anasema mchekeshaji huyo.

 

Cheka Tu ilivyompa mwanga

Ndaro anasema Cheka Tu ilimpata mwanga wa kufanya sanaa na vitu vingine kama kuandaa contents zake mwenye na kuzipeleka YouTube, watu kuzipokea vizuri na kutengeneza maokoto.

Pia Cheka Tu ndiyo sababu ya kupata umaarufu zaidi kwa sababu walimuona ana kitu cha tofauti katika sanaa hiyo.

“ Yaani hata itokee nini siwezi sahau Cheka Tu iliponitoa na wanamchango mkubwa sana kwangu kwa sababu wao ndiyo chanzo cha mimi watu kunifahamu na wamenipa mwanga wa kufanya vitu vingine katika sanaa”

 

Msemo wa ‘au basi’ ulivyoanza 

Ndaro anasema kuwa msemo wake wa ‘Au Basi’ ulitokea tu bila yeye mwenye kujua kama utakuja kuwa msemo maarufu katika jamii, alipata idea wakati yupo location ana-shoot contents zake.

“Nilishangaa sikuwahi kuwaza huu msemo kama utapokelewa hivyo kwa sababu kuna siku nilikuwa location ulinijia tu kichwani nikamwambia mwenzangu tu-shoot kama mimi napita namtongoza yeye ananikalipia halafu namwambia au basi acha tu, basi clip ilivyotumwa mitandaoni kesho yake msemo ukasambaa kwa watu nilishangaa”. Anasema

Ukiacha msemo huo ambao kwa sasa umefunikwa na msemo wake mwingine mpya wa ‘Vina muda basi’ pia alisema kuwa kuna vitu huwa vinakuja na vinapotea.

“Unajua wasichofahamu watu ni kwamba katika tasnia yetu hii unapotoa kitu au ujumbe kufikisha kwa watu kuna muda ujumbe unapotea kutokana na wakati uliopo, sasa unatakiwa uwe mbunifu kwa sababu Wabongo pia hawataki kusikia kila siku msanii anakitu kimoja” Anaeleza Ndaro

 






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Asha Charles


Latest Post