Ndani Ya Boksi: Saa 12 Hadi Saa 12 Na Diamond

Ndani Ya Boksi: Saa 12 Hadi Saa 12 Na Diamond

Wikiendi iliyopita na salio la ‘salare’. Tofauti na leo, niko hoi bin taabani. ‘Lasti wikiendi’ nilihifadhi sura yenye nuru na ‘smaili’ flan hivi. Iliyofanya hata totozi za ‘kijin’zedi’, zione nalipa na kunipa ‘hai’ na ‘hagi’ nyingi.

Saa 12 jioni. Nimetupia ‘snika’ yangu ‘waiti’ chini, jinsi ya ‘daki bluu’. Tisheti ‘waiti’ kifuani inasomeka ‘no dem no koneksheni’. Kapelo, dundo mkononi, uzi shingoni wa silva. Natamanisha kinoma noma yaani.

‘Levo’ ya kutamaniwa na vibaka ni ‘ze sem’ na ‘levo’ ya kutamaniwa na pisi. Dingirai la moto funika vibaya sana mabishoo. Kucheki ni saa 12 kasoro jioni. Nakumbuka nina miadi na mtu mitaa ya Sinza. Duh! Noma.

Nachukua bajaji fasta Sinzani. Ndani ya bajaji goma ni Komasava la Mondi. Suka ana mizuka balaa, nikamchana apunguze sauti. Baada ya simu yangu kuita, mpigaji ni Agnes mtoto wa Joe. Huyu akipiga sina ujanja kabisa.

Naitafuta nusu karne. Ila toka nianze ‘kudeti’ miaka 30 nyuma. Sikuwahi kuzima pumzi kwa pisi kama hii, huyu Agnes hakika ni jini. Akisema kushoto ni kushoto, kulia ni kulia. ‘Sipingagi’ na sitaki ushauri wa mtu kuhusu yeye.

Katikati ya maongezi na Agnes. Suka katoa Komasava kaweka Ukimuona. Ni wazi yule suka ni ‘Timu Mondi Bin Laden’. Agnes akausikia ule wimbo na kuuliza, “Bby naisikia Ukimuona kwani ukwapi? Mh!” Akamalizia na mguno.

Anajua kati ya ngoma zangu tatu basi Ukimuona ipo. Nikajibu nipo ‘bajajini’ naenda zangu Sinza. Nikamtaja mtu ninayemfuata, anamjua. “Ookay baby msalimie Maloto huyo.” Akakata simu na kuniaga kwa ‘kisi’ ya mbali.

Moja kati ya upimbi wa Agnes wangu. Ni uaminifu, mtoto mwaminifu mpaka anakera. Sipendi dem awe mwaminifu sana. Napenda hekaheka, presha na mkwaruzano ya kijingajinga. Sijazoea penzi la amani kabisa.

Dem akikosa makasiriko na kero za hapa na pale. Unakuwa kama ‘unadeti’ binamu yako. Agnes anaamini lolote nikisema, ‘imejini’ anaamini Maloto ni mwijilisti. Kisa nilimwambia jamaa kasoma seminari.
Ndo maana kusikia namfuata Sinza hakuwa na hofu tena. Anaamini nipo katika mikono salama. Hizi dhambi ndogo ndogo sijui nitaacha lini mimi. Ila ‘laifu’ bila kumiliki vidhambi flan ‘softi softi’ sampuli hii siyo poa.

Kidume lazima umiliki dhambi flan flan. Sasa unataka jehanamu aende nani kama siyo wewe? Tumeumbiwa mateso wanaume. Na tunatangulia kudedi sisi kuliko wake zetu, ili tukawe kuni za kuchomea watu kiama.

Nilipofika Sinza na kushuka kwenye bajaji ndipo nikaelewa. Ile bajaji ina picha ya Mondi nyuma na maandishi ya “Simba la Masimba Dangote.” Ndo maana njia nzima ziligongwa pini za ‘Dabiliuu Sibiii Beibi’.

Pale Sinza nilifuata kitabu cha Lady Jaydee. Kuna mwana alipoona kile kitabu nikipewa na Maloto akauliza; “Hivi Diamond hana kitabu chake?” Kuna mwana akamjibu; “Mondi kila siku anaishi kama kitabu tosha, subiri azeeke.”

Tukiendelea na maongezi. Kwenye ile pub flani yenye viumbe uzao wa Zuchu vya kutosha. Mara tunasikia ‘baamedi’ anajibizana na mtu; “Nikutetemekee kwa kipi yaani, wewe Diamond ama?” Anaongea huku kashika kiuno, ngozi kama muhindi wa kuchoma

Tukageuka kumuangalia kwa pamoja bila kuambiana. Saikolojia yangu ipo juu kwa macho tu “nikanoti’ mawazo ya wenzangu. Karibu wote walisema; “Mond ndo wa kutetemekewa? Nchi yetu ina wajinga wengi.” Nikaishia kucheka.

Baadaye tukagundua maongezi yao yalihusu Diamond kabla. Kuna vijana pembeni walikuwa wanamtania yule mhudumu. Kwamba kwa shepu yake amemzidi Zuchu, akijiongeza huenda akawa ‘festi ledi’ wa Wasafi ‘Beibi’.

Sasa kuna mwana kati yao akamtaka dem ashukuru. Eti awanyenyekee wao kwa kumtabiria mambo mema. Ndo bidada akawachana. Kizazi hiki, kwao ni baraka dada zao kupagishwa foleni kimapenzi na mtu mmoja.
Na sababu ya maongezi yale ni baada ya kusikia muziki wa Mondi. Kupitia ile bajaji niliyokuja nayo. Maana Maloto aliyanitonya, kuwa mimi ndo chanzo cha mjadala wa Mondi pale. Kabla sijaja walikuwa bize na tamthiliya.

Muda mfupi baadaye nilikuwa kiwanja kingine. Maloto nilishaachana naye kitambo. Wikiendi napenda mtungi kuliko stori. Maloto mtu wa stori sana angenitoa katika reli ya kulewa, kama ningeendelea kukaa pale.

‘Taimu’ hii nilikuwa chimbo flani hivi la maana. Uzuri wa chimbo hili huwezi kuona ubora wake kama siyo mtu wa mtungi. Wapiga mitungi maeneo yetu hayahitaji mambo flani hivi yale yenye miyeyusho.
Mwanga mkubwa wa taa, kujuana juana hivi. Majiko yenye vyakula kama wali sijui. Kudai pesa kabla vinywaji havijaletwa. Kuletewa bili kila baada ya raundi. Hivi ni vitu wanywaji wenye ‘sivii’ nzito hatutaki kuona.

Nikiendelea kula maji ya Ilala ‘miksa’ na Mbozi ‘Rodi’. Mara ghafla nasikia kelele za watoto wa kike. Tena wengi wamenyanyuka na kuanza kucheza. Nalazimika kurudisha akili sahihi ili niweze kujua wimbo wanaocheza.

“Aliyekuambia kahadithiwa, na aliye kuhadithia kakosea kukwambia... Wala sijafubaa... Tena siku hizi nimezidi utundu, tena nashukuru mashallah rangi kama mzungu, niliyempata kichaa nampa mpaka... ah!”
Ni Zuchu huyo akiwa kashirikishwa na D Voice. Hii ‘vesi’ ya Zuchu inaleta mjadala kwa walevi wenzangu hasa watoto wa kike. Wananena kwa lugha na Mondi katawala mjadala kwa ‘vesi’ hii kuliko mwenye ‘vesi’ na wimbo. Kwanini? Hata mimi sielewi.

Mondi hivi, Mondi vile. Walevi wote stori ni ndoa ya Mondi na Zuchu. Mara wapo wanaosema Zuchu kamchana Mondi. Eti ana mtu mpya anayempa alichomnyima Big Boss wake Mondi. Wapo wanaosema mtoto Zuchu yupo ‘dipu’ na ‘kacha’ ya pwani pwani

Wapo wanaomalizia ile vesi yake kwa tusi flani hivi amazing. Lenye ukakasi na mvuto kwa wakati mmoja. Na hii siyo baa tu mpaka mitaani mitaani ile vesi humalizia na tusi. Zuchu anajua kuandika. Anajua kucheza na kushika dunia ya kizazi cha 2000.

Lakini Simba la Masimba Mondi Bin Laden. Unaweza kuamka asubuhi, giza likaingia mpaka kunakucha tena. Ukajikuta yupo ‘araundi’. Usipomuona mitandaoni utamsikia popote pale. Ni ‘stori meka’. Ameweka mazingira ya kuzungumzika zaidi.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post

Latest Tags