Mitandao ya kijamii ilivyogeuka mtaji kwa watu maarufu

Mitandao ya kijamii ilivyogeuka mtaji kwa watu maarufu

Achana na wale ‘wanaofeki’ wenye kutumia pesa nyingi kwa ajili ya kununua ‘maroboti’ kwenye mitandao ya kuuzia muziki ili kazi zao zionekane zimepata watazamaji wengi zaidi.

Kwenye ulimwengu huu wa kidijitali wapo wakali ambao buku la bando limesaidia kuwasogeza mjini na kuwakutanisha na mashabiki wao, kwa kuwaonesha vipaji vyao na kazi wanazofanya.

Mitandao ya kijamii imekuwa ikileta neema kwa baadhi ya wakali, kwa kuonesha vipaji vyao, kukuza majina yao na biashara zao,  kama ilivyokuwa kwa binti kutoka Afrika Kusini aitwaye Naledi Aphiwe ambaye video yake akiwa darasani anaimba kusambaa kwenye mitandao ya  kijamii hadi kumfika mwanamuziki kutoka nchini Marekani Chris Brown na kuamua kutumia sauti ya binti huyo kwenye wimbo wake uitwao ‘Shooter’ uliopo kwenye albamu yake mpya ya ‘11:11’.

Bongo nako wapo baadhi ya watu maarufu waliotumia mitandao hiyo kutangaza kazi zao na kuzipeleka mjini zaidi hasa wakizingatia kwenye upande wa kukusanya maokoto.

Jackline Wolper ambaye ni muigizaji wa Bongo Movie, amekuwa mmoja wa watu maarufu wanaotumia mitandao kujipatia pesa, licha ya urembo wake lakini hazingatii ‘swaga’ za ‘masista duu’  ku-post picha kali, kwa upande wake hutumia mitandao hiyo kutangaza kazi zake ambazo zinampatia maokoto.

Shilole alipiga jicho kwenye mitandao akajionea fursa ya kutangaza biashara yake ya chakula, huku aki-post baadhi ya wateja wake wanaoenda kupata huduma kwake, jambo ambalo limeendelea kumpatia wateja wengi zaidi kwani baadhi yao hufurahia ‘kupostiwa’ kwenye page ya msanii huyu.

Aunty Ezekiel si kama wale wanao-post wakiwa sehemu za bata huku mezani kukiwa na moja moto moja baridi, kwa upande wake ameamua kupita na upepo wa mitandao ya kijamii kwenye kusukuma kazi zake hasa biashara anazofanya kwa ajili ya kujipatia zaidi wateja.

Yammi, binti anajilia kilaini kwenye ‘lebo’ ya African Princess, inayomilikiwa na mwanamuziki Nandy,  lakini pamoja na yote hayo chimbuko la msanii huyu ni mtandao wa TikTok ambako ndiko alianza kuonesha kipaji chake kwa kuweka baadhi ya nyimbo anazoimba.

Kutokana na kusambaa kwa vipande vya video zake akiimba kwenye mitandao ya kijamii ikawa njia ya mwanamuziki huyu kutambulika kwenye game ya muziki baada ya kusainiwa na Nandy na hadi sasa anaendelea kuachia ngoma mbalimbali.

Misso Misondo, mzee wa umepigaje hapo? misemo yake na ubunifu wa ‘dansa’ wake  wanaocheza wakiwa wamevalia  makoti yenye vumbi nao mitandao ya kijamii imepelekea waweze kupata  shavu katika moja ya kituo cha redio nchini na kujizolea umaarufu mkubwa.

Kufahamika kwao kulianza baada ya video zao wakiwa wanacheza na Dj huyu akipiga muziki kusambaa katika mitandao ya kijamii hasa TikTok.

 

Mandonga Mtu Kazi, ulimi wake uliojaa maneno mengi ulipata ‘sapoti’ kwenye  mitandao ya kijamii, baada ya video zake kusambaa, maneno yake ya kishujaa yenye mbwembwe  yaliwavutia watu wengi  na kupelekea nyota yake kuzidi kung’aa,  na hadi sasa ni moja kati ya mabondia maarufu Tanzania na nchi za jirani.

Chino Kidd, kipaji cheke kama ‘dansa’ na muimbaji kimezidi kupewa nguvu na mitandao ya kijamii  kutokana na juhudi zake za ku-post na kuonesha anachofanya huku akinogesha na msemo wake wa Chino Wana Man ambao kwa mwaka 2023 umeweza ‘kutrendi’ kwa mashabiki wa muziki.

 Jux, baada ya kujiona ana mwili wa kuvalia nguo za aina mbalimbali mkali huyu hakuipiga fursa teke badala yake, kubuni mavazi ya African Boy ambayo amekuwa akiyatangaza kupitia mitandao yake ya kujamii, huku akiwa ameyavaa kwa ajili ya kuvutia wateja zaidi.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Asha Charles


Latest Post