Kipepeo mweusi ya mwasiti kupunguza rushwa ya ngono kwenye sanaa bongo

Kipepeo mweusi ya mwasiti kupunguza rushwa ya ngono kwenye sanaa bongo

Heloow wanafamilia wa Magazine ya Mwananchi Scoop, kama kawaida yetu  kila Ijumaa kwenye jarida hili pendwa upande wa segment ya Burudani tunakuletea habari za kuburudisha  kutoka kwa ma-star mbalimbali.

Week hii tupo na mwanamuziki Mwasiti (Kipepeo Mweusi), ambaye amekuwa akifanya vizuri kwenye muziki kutokana na kipaji chake hasa sauti yake isiyochuja miaka yote na ngoma zake zisizochosha kusikiliza.

Licha ya Mwasiti kufanya vizuri na ngoma zake kama vile ‘Nalivua pendo’, ‘Sio kisa pombe’, ‘Serebuka’ , ‘Kaa nao’ na nyingine nyingi, ameamua kuvuta na kuwasaidia mabinti wenye ndoto kubwa kutokana na vipaji vyao kwa ajili ya kuweza kutimiza ndoto zao.

Kama inavyofahamika kuwa baadhi ya wasanii wa kike wamekuwa wakilalamikia suala la kutakwa kingono wakiwa katika harakati za kujitafuta kimuziki ndivyo, Mwasiti ameona kuna kila sababu ya kutoa msaada kwa mabinti hao wenye vipaji kwa kuanzisha taasisi ambayo ameipa jina lake la ‘Kipepeo Mweusi’ huku lengo kubwa likiwa ni kusaidia na kuokoa vipaji vya watoto wa kike kwa kuwaepusha na rushwa ya ngono.

Taasisi hiyo ya ‘Kipepeo Mweusi’ imezinduliwa rasmi siku ya jana Alhamis kwenye ofisi za THT jijini Dar es Salaam, ikiwa imehudhuriwa na baadhi ya viongozi wa serikali kama vile Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) Dkt. Kedmon Mapana, Gerson Msigwa Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni na Michezo na wengine wengi.

Katika uzinduzi wa taasisi hiyo ya Kipepeo Mweusi, Mwasiti amedai kuwa, haijalenga watoto wa shule bali lengo kubwa ni kwa wale mabinti wanaojitafuta kimuziki.

Anasema Mwasiti, “Kipeo Mweusi ni binti ambaye ana miaka 16 mpaka 30 ambaye yupo kwenye sanaa kiujumla, nia kubwa ya kutengeneza kitu kinachoitwa Kipepeo Mweusi ni kusaidia kutoa elimu ya kuwafanya wasogee zaidi kwenye soko letu la muziki, wasanii wa kike ni wachache sana tunataka watu waongezeke.

Lakini sasa chini wanakutana na vitu ambavyo vinawakatisha tamaa wengine tuliweza ndiyo maana tupo hadi leo wengine walikutana navyo wakashindwa kupenya, kwa hiyo sisi tunaangalia vitu vingi tunajaribu sana kumsaidia binti aweze kupenya na kufikia kwenye ndoto yake kubwa”.

Kama ilivyo kawaida kwa wasanii wengi wa kike kulalamika kukutana na changamoto za kutakwa kimapenzi wakiwa katika harakati za kujitafuta kimuziki ndivyo Mwasiti naye amewahi kukutana  kadhia hiyo.

Anasema Mwasiti , “Wakati niko mchanga kwenye muziki kuna vitu nilipitia  ambavyo kwa njia moja ama nyingine viliniyumbisha, nikasema kuna watu watafurahi nikiyumba nikasema hapana siwezi kuwapa nafasi, na hadi nasema Kipepeo Mweusi ni msichana wa aina hiyo ni kwa sababu kuna vitu hata mimi vilinigusa kwa namna moja ama nyingine.”

Suala la wasanii kupitia changamoto za kusumbuliwa kingono linaonekana kuwa ndiyo chanzo kikubwa cha wasanii wa kike kutokuwa wengi kwenye game ya muziki nchini lakini pia hata wachache wanaopata nafasi wamekuwa hawadumu kwa muda mrefu sokoni.

Lakini kupitia Kipepeo Mweusi Mwasiti ameweza kukusanya takribani wasichana 200 kwa round ya kwanza kwa ajili ya kuwapatia mafunzo, huku nia yake kubwa ikiwa ni kufikia mabinti wengi zaidi.

Mwasiti amedai kuwa mabinti wengi wanaonekana kupenda umaarufu hivyo wengi wakiwa wanajitafuta kimuziki hujikuta wakipewa ujauzito na kutelekezwa na wakati mwingine hupatiwa magonjwa hiyo team nzima ya Kipepeo Mweusi imejipanga kuwasaidia wasichana hao wenye vipaji kwa ajili ya kufanikiwa bila ya kutoa rushwa ya ngono.

Pamoja na kusema hayo Mwasiti ametoa ushauri kwa mabinti wanaojitafuta kwenye soko la muziki nchini

Anasema Mwasiti, “Wito wangu mabinti wasijikatie tamaa kwa sababu hivi vitu vinaongeleka, mwili wako siyo malipo, hutakiwi kulala na producer ili aweze kukusaidia kimuziki wewe mwenyewe jizatiti kwanza unaweza kufanya unacho kifanya”.

 Aidha katika tukio hilo la uzinduzi wa Kipepeo Mweusi baadhi ya mabinti wameweza kukabidhiwa vyeti na mgeni rasmi  wa uzinduzi huo Gerson Msigwa, vyeti hivyo vikiwa ni kutokana na elimu ya fedha na elimu juu ya kuepukana na rushwa  na ukatili wa ngono wakati wakijitafuta kukuza vipaji vyao.






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Asha Charles


Latest Post