Hali ya mwanamuziki wa Singeli Mussa Ramadhan maarufu ‘Dj Mushizo’ inaendelea kuimarika ikiwa ni siku ya nne tangu apate ajali ya moto na kufikishwa katika Hospitali ya Rufaa Amana kwa ajili ya matibabu.
Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu Meneja wa Mushizo, Ally Masupu ameeleza kuwa kwa sasa msanii huyo anaendelea vizuri na matibabu.
“Kwa sasa hajambo anaendelea vizuri, lakini bado tupo Hospitali ya Rufaa Mkoa, Amana. Madaktari bado wanaendelea na matibabu kwani ameungua sana maeneo ya mgongoni na mkononi.
"Madaktari wamemuangalia vizuri moto umeishia nje haujamuathiri ndani, wamesema yupo sawa kabisa. Anaendelea vizuri hali yake inaridhisha tupo naye bega kwa bega kuhakikisha Mwenyezi Mungu anabariki anarudi katika ubora wake,”amesema Masupu.
Aidha akizungumza kuhusu mgonjwa kupewa ruhusa ya kutoka hospitali ameeleza kuwa.
“Hali halisi ya kupewa ruksa yoyote kwa sasa hatufahamu, tupo hapa kuendelea kumuomba Mungu amjaalie kheri lakini tupo tunaendelea na matibabu mazuri tunashukuru sana toka tulivyofika mpaka tunaendelea vizuri. Kwa hiyo kiufupi hakuna mtu anayefahamu ni lini tutapewa ruhusa.
"Mgonjwa anazungumza vizuri japo kwa sauti ya chini na anamfahamu kila mtu anayeingia kwa hiyo ukishaingia ukimuita anaitika na anakufahamu ni flani,”amesema Masupu.
Kuhusu mastaa kujitokeza hospitali
“Kwa sasa kila kitu tunazingatia wenyewe tupo kwenye usimamizi na ubora wa hali ya juu kusimamia kila kitu tukiwa sisi wenyewe kwa hiyo hatuna haja ya kusema labda tunaomba msaada hapana lakini kwa atakayetaka kuja kumuona mgonjwa tunamkaribisha kwa asilimia mia.
"Wasanii waliokuja kumuona ni wengi na siwezi kuwataja kwa majina lakini mastaa waliokuja kumuona ni wengi na wameonesha upendo mkubwa sana wapo ambao amefanya nao kazi na wapo ambao hawajawahi kufanya nao kazi,”amesema Masupu.
Ikumbukwe msanii huyo alipata ajali ya moto nyumbani kwakwe Tabata jijini Dar es Salaam majira ya 12 jioni, Juni 12,2025 huku chanzo cha moto kikitajwa kuwa ni shoti ya umeme.
Nyimbo zilizompa Mashizo umaarufu zinajulikana kwa jina la Wivu pamoja na Mapenzi Hisia, ambazo zinafanya vizuri kwa sasa.

Leave a Reply