Harmonize na Rayvanny waingia mzigoni

Harmonize na Rayvanny waingia mzigoni

Nyota wa muziki nchini, Harmonize na Rayvanny,wametangaza ujio wa ngoma yao mpya ikiwa ni ngoma inayosubiriwa kwa hamu.

Tangazo hilo la ujio wa ngoma hiyo ya pamoja limezua gumzo kwa wadau wa Bongo Fleva, kutokana na historia ya wawili hao kuwahi kuingia kwenye migogoro ya muda mrefu ambayo baadaye walidai kuitatua.

Utakumbuka kuwa Konde Boy na Vanny Boy miaka minne iliyopita waliachia ngoma iliyoenda kwa jina la ‘Paranawe’ ngoma ambayo hadi sasa ina watazamaji 9.9 milioni kwenye mtandao wa YouTube.

Ushirikiano huu ulifanyika wakati wasanii hao wote wakiwa chini ya lebo ya WCB Wasafi kabla ya kuanza kuondoka usafini.

Kuhusiana na ujuo wa ngoma hiyo Harmonize na Rayvanny wote wametangaza kupitia kurasa zao za mtandao wa Instagram. Ujumbe wa Harmonize ulisomeka,

"Hatujawahi kuwa studio kwa zaidi ya miaka 4 lol, ni jambo la kuchekesha, tulikuwa tunangoja hii. Hit nyingine kwenye hii gemu Ijumaa hii na kaka yangu.

“Nitacheka sana nikiwaza vipindi tuliyokuwa hata tukiombeana mabaya kabla hatujajua kuna Mungu na kuna upendo,”ameandika Harmonize.

Hata hivyo, kwa upande wa Rayvanny, ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Lebo ya Next level Music,  kupitia ukurasa wake amechapisha picha inayoonesha chui na tembo porini wakitazamana.

Rayvanny mara nyingi anajitambulisha kama 'Chui' na Harmonize kama 'Tembo'. Ingawa jina la wimbo bado halijafichuliwa, wawili hao walitangaza kuwa itakuwa hit kubwa.

Mwaka jana, wasanii hao wawili waliamua kuweka tofauti zao kando na kuzingatia muziki wao, ambao ulimfanya Harmonize kumkaribisha Rayvanny nyumbani kwake baada ya kupokea tuzo kwa niaba yake. Hatua hii ilimaanisha kuwa tayari wametatua tofauti zao.

Ujio wa ngoma hiyo utakuwa ni baada ya Harmonize kutoa albamu yake hivi karibuni, inayoitwa 'Muziki wa Samia,’.
.
.
.
#MwananchiScoop
#BurudikaNasi






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post