Fanya haya uwe mtu makini

Fanya haya uwe mtu makini

Na Michael Onesha

Mtu wa kwanza kutambua na kuamini kuwa wewe ni wa thamani anatakiwa kuwa wewe mwenyewe. Jione na jiamini kuwa mtu wa thamani kubwa na mwenye vingi, usikubali watu wakuaminishe kuwa mtu wa kawaida usiye na thamani yoyote.

Thamani yako ni matokeo ya kuwa makini katika yale unayoyafanya kila siku katika maisha yako umakini umekuwa changamoto kubwa kwa watu wengi zama hizi.

Tunafanya mambo mengi kwa hisia na siyo kutumia akili na kuweka umakini mkubwa. Kazi nyingi zinazozalishwa zinakuwa zina makosa kwa sababu ya kukosa umakini kwenye kile tunachofanya.

Tumekuwa ni watu wa kukimbizana na ubize wa mambo mengi lakini ufanisi hakuna hata kidogo. Watu wa siku hizi hawezi kufanya kitu kimoja kwa wakati mmoja, utamkuta mtu anakula huku anasoma, anakula huku anaongea na kuangalia TV yaani uwepo wa mtu unakuwa haupo kwenye kile anachofanya ndiyo maana tunakosa kazi makini kwa namna hiyo.

KAMA UNATAKA KUWA MTU MAKINI FANYA HAYA
(i)Kwanza tawala uwepo wako kwenye kile unachofanya
Akili yako iwe unaihamishia kwenye kile unachofanya tu na siyo kitu kingine. Siyo unaandika huku unafuatilia mambo mengine. Unatakiwa kutuliza akili kwenye kitu kimoja kwanza na kifanye kwa ubora bila kutawanya mawazo. Ukiweza kutawala mawazo yako kwenye kile unachofanya utaweza kutawala mambo mengi na kuwa na kazi makini.

(ii)Kagua kile unachofanya kwa mara ya pili
Kabla hujafikisha kazi sehemu husika ikague kwa mara ya pili. Mfano, umeandika kazi, unatakiwa kuiwasilisha sehemu fulani kaa chini isome tena upya, ipitie kuchunguza kama kuna makosa. Kwa namna hiyo utajifunza umakini.

(iii)Jiridhishe kwa kuhakikisha kila kitu kabla na baada ya kufanya.
Hata mtu akikuambia nimefanya kitu fulani penda sana kujiridhisha kwa kuona kile unachoambiwa ni sawa. Ukiwa mtu wa kufuatilia kwenye kila hatua hata dunia itakuwa inakuheshimu kwa umakini wako na kazi zako zitakuwa bora sana.

ILI KUWA MAKINI EPUKA HAYA
(i)Unapofanya kazi yoyote acha vitu vingine kwanza weka akili na mwili wako katika kazi unayofanya
Kama unatoa huduma fulani toa kwa shauku na kuonesha tabasamu kwa mteja wako. Kwa mfano, unaweza kwenda mahali kupata huduma unamkuta mtoa huduma yuko bize na simu, au na Tv umakini wake wote kauweka katika vitu ambavyo si malengo yake ya yeye kuwepo pale.

(ii).kushangaa na kumtafuta mchawi ni nani.

Kutokuwa makini katika kujaza nyaraka mbalimbali, kwa mfano, kila mwaka wanafunzi wanaomaliza elimu ya kidato cha sita huwa wanajaza fomu za kuomba mkopo kupitia bodi ya mikopo. Hivyo kila mwaka lazima wapatikane watu wazembe waliokuwa wanajaza fomu bila umakini wa hali ya juu.
NB
Katika kufanya kazi kwa umakini inahitaji ulipe gharama na gharama yake ni nidhamu ya hali ya juu yaani unatakiwa kujisimamia mwenyewe bila shuruti. Ukiweka ratiba utaamka muda fulani amka na fanya kazi hiyo kwa umakini. Kazi makini nayo inamtambulisha mtu






Comments 0


Leave a Reply

Author

Hello, I'm
Aisha Lungato

A digital journalist and writer for Mwananchi Scoop. My stories are around entertainment, lifestyle, artist profiles and career.


Latest Post